Advertise Here

Tuesday, February 4, 2014

Safu ya James Kalekwa: Ongeza Maana/Thamani kwenye maisha yako kwa kuwa na malengo na kuyaelekea. - Part 5

James Kalekwa
Mifano hai ya watu waliotutangulia

Bwana Yesu
         Bwana wetu Yesu Kristo aliacha enzi na utukufu wake huko mbinguni na kuja duniani kufa badala yetu ili atukomboe kutoka katika laana ya dhambi.Ukitazama katika upana wa yale aliyoyafanya Yesu akiwa duniani utaona kuwa jambo jingine alikuja kuweka msingi wa maisha (kielelezo) ambayo watu wote waliomwamini wanapaswa kuyaishi kwa lugha ya kiiengereza tungeweza kusema Yesu ni role model wa maisha ya imani hii tuliyonayo!

Bwana Yesu hakuishi maisha ya kubahatisha, bali alikuwa na malengo; hebu jiulize nini kilimfanya aanze huduma akiwa na umri aliokuwa nao (miaka 30) na wala si vinginevyo? Kwanini alichagua wanafunzi kumi na mbili na si ishirini, watano au arobaini? Kwanini alikufa wakati huo na si wakati mwingine? (Wakati mwingine Wayahudi walikuja kumkamata Yesu ili wakamshitaki kisha wamuue lakini mwenyewe alisema wakati wake haujafika, akapita katikati yao na kuwaacha)

Ukisoma kwa umakini maombi ya Bwana Yesu kwaajili ya kanisa lake katika Yohana 17:1-26, utaona mambo ya uhakika juu ya vitu alivyokuwa akivifanya mstari 4, "Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye."

Bwana Yesu anaupata wapi ujasiri wa kujua kazi amemaliza wakati alijua wazi kabisa kuwa kuna watu wengi tu walikuwa hawajaokoka bado? alikuwa hajafika sehemu zingine mbali na Mashariki ya kati (Afrika alikuwa bado hajafika,Asia,Ulaya n.k), sasa kwa hali ya kawaida Yesu alikuwa bado hajamaliza kazi lakini malengo yote yanapaswa kuwa na ukomo wa muda.

Hapo baadaye katika sura hii kwa kadri ya neema ya Kristo nitakufundisha mambo yakuzingatia unapoweka malengo na sifa za malengo mazuri. Nakushauri uzisome kwa upya tena injili nne kwa lengo la kutazama maisha ya Bwana Yesu na malengo.

Mtume Paulo
Wafilipi 3:12
"Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwaajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu."
 
2Timotheo 4:6
"Kwa maana,mimi sasa namiminwa,na wakati wa kufariki kwangu umefika.Nimevipiga vita vilivyo vizuri,mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;baada ya hayo nimewekewa taji ya haki,ambayo Bwana mhukumu wa haki,atanipa siku ile;wala si mimi tu,bali na watu wote waliopenda kufunuliwa kwake."

Huwezi kusema umefika au la iwapo hujui unakwenda wapi, vilevile huwezi kukaza mwendo kuelekea kule usikokujua.  “Kuna umuhimu gani wa kupiga mbio, iwapo hauko katika njia sahihi?"

Kuna kitu kinachomfanya Mtume Paulo awaandikie Wafilipi kwamba bado hajafika na anakaza mwendo na anamwandikia Timotheo, mwanae katika imani tuliyonayo kwamba mwendo ameumaliza kwa tafsiri nyingine ni kwamba hakazi tena mwendo; na kitu hicho ni malengo.

Je, wajua Malengo hukamilishwa kwa mikakati???
Sifa kubwa ya malengo ni kuzaa msukumo ndani mwa yule ayabebae wa kuyatekeleza. Kama malengo hayakusukumi kuanza utendaji, bado hayajawa malengo. Hii ni kwasababu malengo hayajikamilishi menyewe bali hukamilishwa kwa mikakati.

Mkakati ni mbinu, hatua madhubuti, wajibu, jukumu… ni utendaji/utembeaji kuelekea kwenye malengo husika. Kwa ujumla wake, mkakati ni mchanganuo wa wajibu/majukumu, wahusika, muda wa utekelezaji na rasilimali zinazohitajika kwaajili ya kukamilisha lengo fulani.

Luka 14:18
"Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumaliza?"

Bwana Yesu anatutambulisha kwenye wazo moja la msingi sana ambalo tunapaswa kujifunza kwalo kwa moyo na nguvu zetu zote. Anazungumza kwa lugha ya kawaida sana kwa kutumia mfano wa Ujenzi.

Hakuna mtu anayeanza shughuli ya Ujenzi bila kukaa chini na kuhesabu gharama na kuona kama anavyo vya kuumaliza! Yesu anaposema “kuhesabu gharama.” Anamaanisha si tu fedha kama ambavyo wengi hudhani moja kwa moja… Unaweza kuwa na fedha lakini huna muda, watu, nguvu kazi, nafasi n.k kwahiyo lazima tuelekeze akili zetu kumuelewa Yesu kwa kina na mapana.

Je, unavyo vya kutosha kukamilisha malengo yako? Jibu la swali huli huzaliwa kwa jinsi ambavyo utatumia muda kufanya uchambuzi na kutengeneza mkakati.

Kuna watu wengi sana nimewashuhudia na marafiki zangu kadhaa wamenaswa kwenye mkwamo ambao hata mimi hapo awali nilijikuta nimekwama na hata sasa ninajuhudi za kupigana vita kepuka mkwamo huo… kuanza jambo na kutolikamilisha!

Mkakati unakusaidia kujinasua kutoka kwenye mkwamo huo. Ninaomba uambatane nami kuchanganua mambo muhimu ndani ya mkakati.

Wajibu/Jukumu – Huu ni mchanganuo wa kazi ndogo ndogo ili kulielekea lengo husika 
Wahusika – Ndani ya mkakati unapaswa kuainisha nani atahusika kufanya nini. Ni muhimu sana mkakati ufikie hatua ya kugawa majukumu na wajibu kwa muhusika fulani kwaajili ya utendaji. Kutokana na aina ya malengo, vyaweza kuwepo vigezo vya kumbebesha mtu fulani wajibu au jukumu: mfano upatikanaji wake, kipaji, uwezo, uzoefu, ujuzi n.k

Muda/Wakati – Hii ni rasilimali muhimu amabayo kila mtu amepewa sawasawa. Kila mtu ana masaa ishirini na nne  (24) ndani ya siku moja, siku saba ndani ya wiki moja. Kinachojenga tofauti miongoni mwetu ni namna tunatumia muda wetu.

Ni LAZIMA ufanye maamuzi ni muda kiasi gani utahitajika kwaajili ya kuleta utimilifu wa jukumu fulani. Usidhani utafanya jambo moja muda wote! Kwahiyo, ni lazima kwa mfano kusema “Nitaandaa rasimu ya mafundisho/kitabu ndani ya wiki ya kwanza ya mwezi wa pili yaani tarehe 1- 7 Februari.”

Au unaweza kutumia Mchanganuo wa jedwali kama nilivyofundisha hapo awali na nitaweka mfano huo tena baada ya Maelezo haya juu ya mkakati. Usipochanganua muda hiyo ni dalili ya kuanza kutumia vibaya muda wako, utaanza kufanya chochote wakati wowote… jukumu la tisa utaanza nalo, utajikuta unatamani kufanya jukumu la nne, mara unaona jukumu la saba linaibuka likifuatiwa na jukumu la kwanza.

Hutakuwa na mtiririko maalum! Kwahiyo utajikuta katika ya mwaka hujafanya chochote cha maana zaidi ya kurukaruka tu huku na kule.

Rasilimali fedha – Masikioni mwa watu wengi sana ukisema rasilimali, huja Taswira ya fedha. Lakini kwangu binafsi hii huja kama rasilimali ya mwisho… Kwa mfano, unadhani unahitaji fedha kiasi gani kuandika kitabu???

Hauhitaji hata senti moja kuandika kitabu ila kuchapisha kitabu ndiyo unahitaji pesa… Sasa,  ni hekima sana kujua ya kwamba kabla ya kitabu kuchapishwa, kwanza huandikwa! Kwahiyo, usisingizie fedha… Kaa chini uandike. Anza kufanya yaliyo ndani ya uwezo wako kwanza.

Mkakati mzuri ni ule ambao hukusukuma kufanya Mchanganuo wa rasilimali fedha. Hii hupelekea kujua ni fedha kiasi gani zitahitajika ili kukamilisha jukumu fulani. Lakini zaidi ya hapo ni lazima kujua kiasi hicho cha fedha kitahitajika kwa wakati gani.

Vilevile, ni muhimu kuainisha vyanzo vyako vya mapato (jinsi gani fedha hiyo itapatikana) – mshahara, faida ya biashara, gawio, mkopo, changizo (harambee), ufadhili n.k hii itakusaidia sana kutembea kwa Uhakika na kutoshangazwa na mambo mengi (not to be caught by surprise).

Nguvu kazi – Huu ni uwezo ulifichika ndani ya mtu (hazina). Uwezo huu huyaleta mawazo katika uhalisia… Husababisha vitu kuwa halisi. Ni mjumuisho wa ujuzi, Uzoefu, ufahamu na nguvu. Kwa mfano, ili uwe na kitabu au mafundisho kama haya ni lazima uandishi, mitindo ya uandishi na utumuzi wa lugha viingie kazini.

Lazima kalamu na karatasi au ipad, kompyuta mpakato n.k vitumiwe na mtu ili kuzalisha matokeo. Ile Akili, fikra na mawazo ndiyo nguvu kazi. Lazima mkakati wako ukusukume kutambua na kuyachambua haya kinagaubaga.

Kumbuka, unafanya uchambuzi wote huo kwa lengo kuu la kujibu swali Je, unavyo vya kutosha kukamilisha ujenzi wa mnara?

Hongera, sasa waweza kufanya tathmini!
Huwa ninapenda chanagamoto moja… Je, ni wakati gani sahihi kusema “huu ni mwaka mpya”? Je, ni mwanzo au mwisho wa mwaka? Wengi husema mwaka ni mpya mwanzoni mwa mwaka, nadhani kwasababu ya kubadilisha kalenda. Lakini kimsingi, mwaka unakuwa mpya au la baada ya kuwa umefanya tathmini… na tathmini hufanyika mwishoni mwa mwaka.

Ninachotamani kujenga ndani ya moyo wako ni kwamba kila baada ya msimu, muda au wakati fulani ambao mwenye malengo amejiwekea, ndipo Uhitaji wa kufanya tathmini! Tathmini ni tafakari ya ndani kuhusiana na malengo ambayo umejiwekea. Lazima ujipime ni kwa kiwango gani umeyafikia malengo husika.

Kama umeyafikia lazima ujiulize mambo ambayo umejifunza, mambo yatokanayo, na mengineyo kutoka kwenye malengo hayo. Vivyo hivyo kama hukufanikiwa kuyafikia malengo yako.

Maisha ya vijana wengi wa zama zetu, hata baadhi ya watoto wa Mungu (watu waliookoka) huwa hawafanyi tathmini. Kwahiyo wanajikuta wakitembea vilevile kila siku. Huwezi kufanya tathmini mpaka umekuwa na malengo!

Kwa ujumla wake, kutathmini ni KUJIPIMA! Na hii yote hukupa kujitambua, kufahamu wazi wazi juu ya mwenendo/njia zako.

Hagai
“Zitafakarini njia zenu,"
“Lengo”  si kuwa na malengo bali kuwa na matokeo:

Kitu cha muhimu kufahamu baada ya kuweka malengo yako vizuri na kuainisha jinsi gani utayafikia yaani dhima(mpango),basi napenda kukumbusha kulenga matokeo na si kulenga dhima/mpango. Maana yangu ni kwamba usifanye tu utekelezaji eti kwa vile ndivyo ulivyouainisha,bali lenga kuleta matokeo yanayoonekana na yanayodumu.

Kwa kutumia mfano wetu wa kuihubiri injili kwa watu 1000 nchini Tanzania katika wilaya 4 kwa mwaka,usihubiri tu ili kufikia watu 1000,kisha iweje?kwahiyo lazima ulenge matokeo,baada ya hapo nini kinafuata.Siyo watu 1000 kwa lengo la kuja kuandika wakati wa tathmini,kumbe hakuna matunda yoyote.Bwana Yesu alilenga matokeo ndiyo maana matunda yake yapo mpaka hivi leo.Lenga kuleta matokeo wala si kukamilisha mipango!

Usuri wa malengo: Ufahamu wa ndani zaidi
Ndugu msomaji na mfuatiliaji wa mafundisho yetu, kama ungetamani kuona maisha yako yakiwa na matunda na maana sana. Ninakushauri utafakari sana juu ya kufanya uamuzi wa kumwamini Yesu Kristo, yaani kuokoka. Hii si dini wala dhehebu, bali ni kumwamini Yesu moyoni na kumkiri, sawasawa na neno lake, kisha kutembea sawasawa na ukiri huo. Yesu ameyapa maisha yetu thamani kubwa na yeye ndiye chanzo cha hekima, maarifa na ufahamu wote. Hivyo, ukiokoka ni mtaji mkubwa sana kuyaishi mafundisho haya.

Pia, kama utahitaji kumwalika ndugu James Kalekwa kuwa mwalimu, mnenaji, mwezeshaji kwenye kongamano, warsha au semina; ama unahitaji kujua namna gani ya kupata vitabu au mafundisho zaidi… Fanya hivyo kupitia mawasiliano yaliyoambatanishwa katika tovuti hii.

- Mwisho wa Somo -

 Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764

Monday, January 27, 2014

Safu ya James Kalekwa: Ongeza Maana/Thamani kwenye maisha yako kwa kuwa na malengo na kuyaelekea. - Part 4

James Kalekwa
R  -(Realistic). Lengo zuri lazima liwe na uhalisia, ambao huja kutona  na kuangalia hali halisi ya pale ulipo, majukumu na nafasi yako. Mfano mzuri ni huo hapo juu kwenye sifa ya kufikika. Unapoweka malengo juu ya jambo fulani haimaanishi kwamba umeacha kufanya mambo mengine.

Unapoweka malengo ya kihuduma haimaanishi kuwa umeacha kuwa baba au mama (kama Mungu amekupa watoto) kwahiyo usijitoe kwenye wajibu mwingine uliopewa na Mungu, haimaanishi kwamba utastaafu kuwa mme au mke (ikiwa umeoa kama mimi au umeolewa), haimaanishi kwamba wewe si mtoto wa wazazi wako (ikiwa bado wa hai) kwahiyo unawajibu huo.

Lakini jambo jingine la msingi kufahamu, ni je, utapata muda wa kutathmini kazi yako au unaenda kienyeji kienyeji tu, Je, utapata muda wa kufuatilia mavuno hayo na kuyaombea au kuyalea (hakuna umuhimu wa kuzaa kama huwezi kulea), Je kuna mafundisho ya kutosha kwa watu hao? Lazima uzingatie kanuni ya kuwa mkweli juu ya nafsi yako?

Watoto wengine wa Mungu wamekwama sehemu si kwasababu hawana Yesu. Yesu wanae, Roho Mtakatifu yupo pamoja nao na wanaenda mbinguni lakini wamekwama sehemu kwasababu hawana maarifa juu ya jambo hilo. Mtumishi mmoja wa Mungu aliandika, "Upako unaletwa na maombi lakini maarifa ya neno huja kwa kusoma.

Maombi kamwe hayawezi kufuta ujinga na kukupa maarifa. Neno la Mungu limeweka bayana kuwa watu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa Hosea 4:6. Ina maana upako siyo tiketi ya kukuzuia kuangamizwa kama huna maarifa ya neno la Mungu."



T  -(Time bound). Kitu cha kuzingatia katika kuweka malengo ni swala la muda, yaani tamati ya malengo husika. Hii itasakusaidia sana kupima mafanikio na kuweza kufanya tathmini juu ya maendeleo wakati wote wa utekelezaji wa malengo husika. Hebu fikiria nini kilimfanya Bwana Yesu aseme “…hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.", kwasababu malengo yake yalikuwa yamefungwa katika muda wa kuyakamilisha, alikuwa anaujua mwisho tangu mwanzo, kama ni msafiri basi alikuwa anajua stendi au kituo cha mwisho cha safari yake.

Hebu jiulize nini kinaweza kutokea kama malengo yako hayatakuwa na muda wa kuyaona yakitimilika, ”time of their realization.”?. Ngoja nikupe mfano wa kawaida sana ndipo utaelewa nini ninamaanisha, hebu fikiri pamoja na mimi itakuwaje kama mwanafunzi wa darasa la tano akibakia darasa hilo siku zote, bila kuhitimu wala kwenda darasa jingine, siku zote ni darasa la tano?

Ingefika wakati mwanafunzi huyu angechoka na masomo kwasababu hayana mwisho, lakini pia mzazi wake pia angechoka kulipia gharama za kitu kisicho na ukomo au utimilifu. Maana yangu hapa ni kwamba kinachomfanya mwanafunzi wa darasa la tano asome kwa bidii ni kwasababu kuna darasa la sita mbele na la saba yaani kuna kipindi cha kuhitimu hatua husika ya masomo la sivyo asingesoma kwa bidii.

Hebu fikiri nini kitatokea kama inatokea wanawake wanakuwa wajawazito siku zote, bila mwisho!!! Najua wengine wasingetamani kuwa na hali hiyo, kwasababu hakuna kuhitimu hali hiyo, yaani kujifungua.


Mfano wa lengo ambalo ni SMART: Kuihubiri injili kwa watu 1000 nchini Tanzania katika wilaya 4 kwa mwaka mmoja.


Je, lengo hilo ni hususani (Specific)? Ndiyo kwasababu limetaja idadi ya watu,idadi ya wilaya na nchi.

Je, lengo hilo Linapimika (Measurable)? Ndiyo kwasababu ya idadi, eneo la kijiografia (mahali) yaani mwisho wa siku unaweza kukaa chini na kuangalia kama wilaya 4 zimefikiwa na kwa kiasi gani, vilevile kuona kama watu 100 wamefikiwa.


Je, lengo hilo linafikika (Attainable)? Ndiyo, kwa Jiografia ya Tanzania inawezekana kuzifikia wilaya hizo kwa muda huo. Pia unaweza kupata muda wa kujiandaa, kifedha, kimaombi, ujumbe kwani mwalimu mzuri ni mwanafunzi wa kudumu, kwahiyo lazima ujifunze ili ukafundishe.


Je,lengo hilo linauhalisia  (Realistic)? Ndiyo, kwasababu muda unaruhusu kufanya mambo mengine kama maandalizi ya uwanja/ukumbi wa mikutano, mahali pa kufikia, watu wa kushirikiana nao (si unajua huwezi kushirikiana na watu wote na kwa upande mwingine huwezi kushirikiana na kila mtu?) n.k yaani kwa lugha ya kiingereza wanaita "logistics", pia unaweza kuwa na muda wa kutimiza wajibu wako mwingine kama baba/mama (mzazi), kama mme/mke, kama mtoto na vitu vya msingi kama hivyo lakini pia kuna jambo la muhimu ambalo watu wengi hulipuuzia,lakini ni la muhimu sana.

MAPUMZIKO! Mungu baada ya kutenda kazi siku sita alipumzika! Umuhimu wa kupumzika ni kwamba unaporudi tena kwenye utekelezaji, unakuja na nguvu mpya "fresh". Mungu akusaidie kuyaelewa haya na kuyatendea kazi na maisha yako hayatakuwa kama yalivyo, na hayo ndiyo maombi yangu kwa Mungu kwaajili yako msomaji wangu.

Somo litaendelea Jumatatu Ijayo.....

 Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764

Monday, January 20, 2014

Safu ya James Kalekwa: Ongeza Maana/Thamani kwenye maisha yako kwa kuwa na malengo na kuyaelekea. - Part 3

James Kalekwa
Kwahiyo, somo hili litaanza kwenye mzunguko wa malengo na ni wajibu wako kujua kusudi lako, maono na dhamira yako.
 Ninaanza kwa kuamini kwamba (based on the assumption that), wewe, ndugu msomaji wangu, umekwishawekeza muda wako kulitafuta kusudi la Mungu juu ya maisha yako, unayajua maono yako na umeyafikisha kwenye hatua ya dhamira (utume).

Malengo ni nini?
 Binafsi nimekuwa na changamoto kubwa sana kutafuta maana rahisi na ya kueleweka juu ya neno “malengo.” Huwa ninawaambia watu wengi ya kwamba inawezekana kwamba usiwe na maana (definition) ya malengo, lakini ukiyaona ni lazima utayafahamu.

Lakini, huwa ninaamini ya kwamba huwezi kuanza kutenda/kushughulika na kitu, jambo au hali usiyoijua. Na kwa misingi hiyo basi, ninawiwa kujenga ufahamu ndani yako juu ya malengo. Katika mzunguko niliouonyesha hapa awali kwenye taswira, malengo huzaliwa kutoka kwenye dhamira (utume).

Lazima dhamira ikusukume kuumba malengo! Sasa, malengo ni nini basi? Malengo ni ajenda au mahitaji husika/mahususi ambayo mtu fulani hujiwekea kwa kipindi cha muda fulani ili kumzalishia matokeo yanayoonekana, matunda na/au mabadiliko yaliyokusudiwa… hupimika, huweza kufanyiwa tathmini!

Weka malengo kwa vigezo hivi:
 Malengo mazuri huwa na sifa ya “SMART”, neno la kiingereza linalomaanisha nadhifu, -enye uelewa mzuri. Kwahiyo malengo yako yanapaswa kuwa nadhifu, sasa neno smart linabeba maana kubwa sana kwa kila herufi yake:

S   -(Specific), kwanza lazima lengo liwe ni maalum au hususani juu ya jambo, mtu au hali fulani. Kwa mfano mtu anaposema, “Mimi ninataka kupambana na umaskini.”. Ni sawa hilo ni lengo lakini si hususani, yaani halina mwelekeo… Je, mtu huyo anataka kupambana na umaskini wa aina gani (umaskini wa kifikra, kifedha…), Je, anapambana nao katika ngazi ipi? (mtu binafsi, kijiji, familia, nchi…) lazima uainishe.

Na ndivyo ilivyo katika huduma, unaweza kusema nina wito wa kuhubiri injili, ni sawa lakini ni katika ngazi gani? Ni wazi kwamba kuizungukia dunia yote ni jambo ambalo si rahisi (nchi zote, mikoa yote, majimbo yote, wilaya zote, vijiji vyote na kaya zote za dunia.) Si jambo rahisi, ukijaribu utaumia tu na matunda hayatakaa.

Mfano: Lengo langu ni kuihubiri injili nchini Tanzania.
Kumbuka kuwa Tanzania ni nchi kubwa, ina mikoa zaidi ya ishirini na wilaya zake na tarafa, kata, mitaa/vijiji na kaya (familia) kwahiyo unatakiwa kuwa specific zaidi. Kwahiyo waweza kusema, kuhubiri injili nchini Tanzania katika ngazi ya wilaya.

M   -(Measurable), Pili lengo lolote linatakiwa kupimika, Je unaweza kuuona ufanisi, matokeo au matunda ya lengo hilo? Kwa mfano lengo la kuihubiri injili nchini Tanzania katika ngazi ya wilaya…Baada ya muda je unaweza kupima matokeo ya lengo hilo.

Sasa kuna njia mbalimbali za kuyapima malengo yetu, baadhi ya njia ni kuangalia mabadiliko katika maisha ya watu, je, kuna mabadiliko yoyote,njia nyingine ni kuangalia je, idadi iliyokusudiwa imefikiwa? Tukiendelea kuutumia mfano wetu wa kuihubiri injili nchini Tanzania katika ngazi ya wilaya ili tuufanye kuwa SMART; Ili kuweza kupima lengo hilo waweza kusema:
Kuihubiri injili kwa watu 1000 nchini Tanzania katika wilaya 4 (unapaswa kuzitaja wilaya ulizokusudia kuzifikia) kuanzia Januari mpaka Juni.

Je, unaweza kuyapima matokeo ya lengo hilo? Kwasababu unaijua idadi ya watu unaotaka kuwafikia ni watu 1000 na tayari unajua wapi pa kuwapata (wilaya 4, Tanzania) kwa maana hiyo basi ni watu 250 kwa kila wilaya. Kwahiyo hatimaye unaweza kuangalia Je, hizo wilaya 4 zilifikiwa na injili na Je, watu 1000 walifikiwa pia? Hivyo ndiyo kupima malengo!

A    (Attainable), Jambo jingine la tatu na la msingi kufahamu ni kwamba lengo lolote linapaswa kufikika. Hapa unapaswa kuangalia kwamba Je ,ninao uwezo wa kukamilisha lengo hilo kwa kiwango hicho, Je,ninao watu wa kushirikiana nao kufika huko,Je ninahitaji maandalizi ya kimaombi, kifedha, kifursa n.k kiasi gani?

Kuna malengo mengine ukiyatazama unatambua tu kwamba mtu huyu anaota ndoto za mchana, kwa kutumia mfano wetu wa injili nchini Tanzania, unakuta mtu anasema: Lengo langu ni kuihubiri injili nchi yote ya Tanzania kwa mwaka. Hilo ni lengo zuri na lina nia njema lakini Je, unaweza kuifikia nchi yote ya Tazania kwa mwaka? maana yake mikoa zaidi ya 20, yaani wastani wa wilaya 5 kila mkoa, sawasawa na wilaya 100. Mwaka una siku 365, ambapo ni sawasawa na wastani wa siku 3 kila wilaya.

Unaweza? Vipi kuhusu  muda wa kujiandaa? gharama? familia? mapumziko? Usafiri,si unajua wakati mwingine inachukua siku nzima kusafiri toka mkoa mmoja kwenda mwingine? Mikutano hiyo au huduma hiyo utaiandaaje? Je, lengo hilo linafikia?, basi hata kama likifikika halitakuwa na ufanisi.

Somo litaendelea Jumatatu Ijayo.....

 Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764

Friday, January 17, 2014

Papa Francis atimua Makadinali.

MAKADINALI wote isipokuwa mmoja waliokuwa wakisimamia benki ya Vatican wamefutwa kazi na Papa Francis. Waliokumbwa na ‘fagio hilo la chuma’ ni makadinali wanne ambao ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje, Kadinali Tarcisio Bertone SDB, Kadinali Odilo Scherer kutoka Brazil, Telesphore Toppo kutoka India na Domenico Calcagno kutoka Vatican.

Kadinali Jean-Louis Tauran ambaye ni Mkuu wa Baraza la Upapa linalohusika na Mijadala ya Kidini, amenusurika kwa mujibu wa gazeti la kila wiki la Kikatoliki la The Tablet.

Gazeti hilo lilieleza jana kuwa isipokuwa Calcagno, makadinali hao wote ndio kwanza walikuwa wametimiza miezi 11 tangu wateuliwe katika kipindi cha pili cha miaka mitano, wakiwa wameteuliwa na Papa Benedict XVI muda mfupi kabla ya kujiuzulu.

Benki hiyo ya Vatican ilikumbwa na kashfa ya utakatishaji fedha mwaka 2010 baada ya waendesha mashitaka wa Italia kugundua shughuli zenye shaka zihusuzo fedha chafu ndani ya benki.

Mwenyekiti wa Benki hiyo, Ettore Gotti Tedeschi na naibu wake, Paolo Cipriani walichunguzwa baada ya polisi kukamata euro milioni 23 kutoka kwenye akaunti ya benki hiyo.

Ilidaiwa kuwa ingawa benki hiyo ilikuwa inadai kupambana na utakatishaji fedha, ilivunja sheria kwa kujaribu kuhamisha fedha hizo bila kutambulisha mtumaji wala mpokeaji, au zilikuwa zinatumika kwa shughuli gani.

Tuhuma hizo zilikanushwa kwa nguvu zote na Vatican. Papa Francis ameteua makadinali wengine kuziba nafasi za aliowatimua na kuunda alichokiita Tume ya Makadinali ya Kusimamia Taasisi kwa ajili ya Kazi ya Dini (IOR), ambao ni makadinali Christoph Schönborn (Vienna), Thomas Collins (Toronto); Santos Abril y Castillo´ (St Mary Major) na Kadinali Pietro Parolin (Waziri wa Mambo ya Nje).

- Habari Leo -