Advertise Here

Thursday, January 9, 2014

Mwimbaji wa Nyimbo za Injili Nchini Nigeria anusurika kifo.

I don’t care, whether you like me or my music -Busola Oke
Queen Eleyele

Mwimbaji maarufu wa Nyimbo za Injili toka Nchini Nigeria Busola Oke maarufu kama Queen Eleyele anusurika kufa kwenye ajali mbaya ya gari iliyotokea January 4, Mwaka huu akitokea Oyo Estate kuelekea Lagos.

Baada ya Ajali hiyo kutokea, watu waliokuwa eneo la tukio waliwahi haraka eneo la tukio na kumchukua Mwimbaji huyo kisha kumpeleka hospitalini.

Hata hivyo gari iliyokuwa ikiendeshwa na Mwimbaji huyo iliharibika vibaya.
http://4.bp.blogspot.com/-oGgP2XlVC4I/Us12M0h_mzI/AAAAAAAABxs/N1YkkEyXpK8/s1600/bubu.jpg
Hii ni Video ya wimbo wa Queen Eleyele ujulikanao kama Afefe Ife

Wednesday, January 8, 2014

Kanisa la Moravian Mkoani Mbeya latoa Msaada kwa watoto yatima.

Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Kusini Magharibi Ushirika wa Chunya Mjini, limetumia zaidi ya Sh6 milioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya shule kwa watoto 100 yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi.
 
Akikabidhi msaada huo jana mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Deodatus Kinawiro, Mchungaji wa Kanisa hilo Anyandwile Kajage alisema kuwa fedha hizo zilitumika kwa ajili ya ununuzi wa sare za shule, madaftari, viatu na chakula.

Kajage alisema kuwa lengo la kutoa msaada huo ni sehemu ya hamasa kwa watoto walio katika makundi hayo ili kuwajengea mazingira mazuri ya kuishi kwa amani na faraja.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro alipongeza jitihada za wadau na waumini katika kutoa misaada na kuitaka jamii kujitolea kwani kutoa ni moyo na siyo utajiri.

Alisema amefarijika kwa kiasi kikubwa kwa mwamko wa madhehebu ya dini kwa kutambua uhitaji wao kwa kukabiliana na janga la ongezeko la watoto wa mitaani na kuzitaka asasi nyingine za kiraia kuiga mfano huo.

Naye Mtoto Salome Zumbe alilishukuru kanisa hilo kwa kutoa msaada huo na kwamba utakuwa ni chachu na kichocheo cha wao kufanya vizuri katika mitihani yao na kuzingatia masomo ili kuweza kuendelea katika elimu ya ngazi za juu.

- Mwananchi -

Tuesday, January 7, 2014

Safu ya James Kalekwa: Ongeza Maana/Thamani kwenye maisha yako kwa kuwa na malengo na kuyaelekea. - Part 1

James Kalekwa
Mithali 29:18, “Pasipo maono, watu huacha kujizuia…” 
Habakuki 2-3, “BWANA akanijibu, akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili kila aisomaye apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingoje; Kwakuwa haina budi kuja, haitakawia.”

Salamu za mwanzo wa Mwaka
 Ndugu msomaji na mfuatiliaji wa mafundisho yetu kwa njia ya mitandao, pokea salamu za heri ya mwaka mpya kwa jina la Yesu Kristo kutoka kwangu na mke wangu kipenzi, Frida. Tumekuwa na shauku sana kukushirikisha mafundisho haya na tumeomba sana kwaajili yako. Kiu iliyojaza mioyo yetu ni kuona unatembea na kuliishi kusudi la Mungu kwenye maisha yako binafsi, familia, jamii na kisha uweze kuepika (influence) taifa letu kwa ujumla.

Pia, tunaomba upatapo muda tafadhali omba kwaajili yetu tunapotekeleza wito tulioitiwa wa kuwakamilisha watakatifu kwa njia ya mafundisho. Mwaka huu tunataraji kuona wigo ukifunguka zaidi na mikoa na wilaya nyingi hapa kwetu
tutawafikia kwa mafundisho ya neno la Mungu. Kumbuka kuomba kiwemo chakula cha kutosha ghalani!

Sasa, nikukaribishe uungane nasi kwenye mfululizo huu mpya juu ya kuongeza thamani ya maisha yako kwa kuwa na malengo na kuyaelekea.

Lengo kuu la somo:
Kumuwezesha mtu binafsi kuwa na ufanisi na mwelekeo katika maisha ya siku kwa siku.

Malengo mahususi ya somo:
        i.            Kuelekeza kwa upana juu ya usuri (essence) wa maisha yenye malengo.
     ii.            Kujifunza kutoka kwenye maisha ya waliotutangulia juu ya malengo na kumahalisha (contextualize) mafunzo hayo.
   iii.            Kujenga stadi na mbinu za kuweka, kutekeleza na kutathmini malengo kwa mtu binafsi na vikundi.
   iv.            Kumuandaa mtu binafsi kwaajili ya kuwa chachu ya mabadiliko kwenye taifa.

Ni Muhimu sana ukatunza kumbukumbu ya malengo hayo ili uyapime na ujipime kulingana nayo wakati wote wa mfululizo huu.
Ndugu, imekuwa ni desturi miongoni mwa watu wengi sasa kila ifikapo mwanzo na/au mwisho wa mwaka au msimu fulani kuwasikia wakisema, wakielekeza na wakikumbushana juu ya kuwa na malengo kwenye maisha. Mijadala ya namna hiyo si maarufu sana katikati ya mwaka na wengi hawajisumbui kuyaelekea wala kutathmini hayo malengo – hilo ni tatizo kubwa. Nasi kwa neema ya Mungu, tumeiona ni vyema tuanze mwaka huu kwa kukukumbusha na kukuelekeza juu ya hilo, si kama desturi, kwa kuwa ni shauku yetu kuona unakuwa na kustawi… Karibu ujifunze, si kama desturi.

Hebu jiulize pamoja na mimi juu ya mambo haya:
Kisa mkasa (Scenario) #1. Msafiri asiyejua aendako:

Nimewahi kuzungumza mahali pengi na kwenye kitabu changu cha “Wokovu ni uhakika wa maisha ya Sasa na ya Baadaye.”  Juu ya mfano huu… Hebu jaribu kufikiri ukiwa katika stendi kubwa ya mabasi yaendayo katika mikoa mbalimbali (mfano stendi ya Ubungo- Dar Es Salaam, Nyegezi/Buzuruga- Mwanza, Msamvu- Morogoro n.k) Anatokea mtu mmoja ambaye kwa mwonekano wake ni msafiri… amebeba mabegi na mizigo kadhaa, mkononi ameshikilia chupa ya maji ya kunywa… akakujia kisha akakuuliza, “Ndugu, naomba unionyeshe basi kwani ninataka kusafiri.”

Je, utamuonyesha basi gani? Au utamuonyesha basi la kwenda wapi?...
Kwa kadiri nijuavyo mimi ni kwamba mtu mwenye akili timamu na nia njema, kama wewe ndugu msomaji wangu, utahitaji kupata maelezo kamilifu… utataka kujua kule anakoelekea yaani mwisho wa safari yake ili umwonyeshe basi linaloelekea mwisho huo.

Sasa iwapo ukimuuliza swali hilo kisha akakujibu kwamba “ndugu, sijui kule ninakokwenda.”  Je, utamuonyesha basi liendalo wapi? Au utamwonyesha basi gani? Huwa ninaamini na kushawishika kabisa ya kwamba wewe hutakuwa na kosa utakapomwonyesha basi lolote ili aende kokote kwasababu hajui kule aendako! Kwahiyo kokote atakapopelekwa ni sawa.

Somo litaendelea Jumatatu Ijayo.....

 Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764

Tuesday, December 10, 2013

Cheka na Mc Pilipili - Episode 3.

Leo ni Siku ya Jumanne na Kama kawaida siku ya Jumanne huwa tuna kitu kinaitwa "Cheka na Mc Pilipili".

Hivi unatambua kuwa Mc Pilipili ni Muhubiri na ni Mchungaji??? Sasa leo katika "Cheka na Mc Pilipili" tunakuletea moja ya Mafundisho ya Neno la Mungu ya Mc Pilipili, alipofundisha kupitia Kipindi cha Gospel Hits cha Sibuka Tv.

Haya Kazi kwako sasa kutazama

Monday, December 9, 2013

Mchungaji Gwajima kuhubiri Injili kwa Helikopta.

WAKATI viongozi wa madhehebu ya dini ya Kikristo nchini, wakionekana kushindana kwa utajiri, hali inayowafanya waishi `kifalme’ na kufungua miradi, Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amesema hana mpango wa kufungua biashara, zaidi ya kujikita na mahubiri ya Injili.

Aidha, amesema Mungu anaendelea kumbariki katika kazi yake, ndiyo maana mambo yake yanamnyookea, akitolea mfano kuwa baada ya kumiliki nyumba, magari na fedha za kutosha, sasa amembariki na kumpa helikopta atakayoitumia kufikia waumini wake wa ndani na nje ya nchi.

Usafiri huo wa angani, utaongeza idadi ya vyombo vya usafiri vya Mchungaji huyo, ambaye anatajwa kuongoza kwa utajiri miongoni mwa viongozi wa madhehebu ya Kikristo nchini, kwani anamiliki magari kadhaa, likiwamo lakifahari aina ya Hummer lenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 200.

Akizungumza na gazeti hili hivi karibuni kwa simu, Gwajima ambaye alikuwa anaendesha mikutano ya kueneza Neno la Mungu katika mikoa mbalimbali ikiwamo Kilimanjaro na Tanga, alisema helikopta imeshanunuliwa na matarajio yake ni kwamba, baada ya kukamilika taratibu zote za kisheria nchini, itawasili.

“Sipendi kusema mambo yangu sana, lakini kwa kuwa umeuliza naweza kugusia kidogo, ni kweli nina mpango wa kuanza kuhubiri Injili kwa helikopta, na kama ilivyo kwa gari, nayo hii nimepewa na watu wa Mungu walioguswa na huduma yangu Japan."

“Itafika nchini wakati wowote mambo ya kisheria yakikamilika, huu si wakati wa kuizungumzia sana maana bado haijafika,” alisema Gwajima ambaye gari lake aina ya Hummer liliwahi kuzua gumzo, wengine wakimhusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya, ingawa anapuuza madai hayo.

Mchungaji Gwajima, alieleza wazi kuwa utajiri wake unatokana na baraka anazopewa na anaowahudumia ndani na nje ya nchi na pia kazi yake ya kufundisha anayoifanya ughaibuni.

Aidha, kutokana na utajiri anaosema unatokana na baraka za Mungu, Mchungaji Gwajima anamiliki nyumba ya ghorofa nne eneo la Mbezi Beach katika Manispaa ya Kinondoni, ingawa haijakamilika.

Pia, amewanunulia wachungaji wake 40 magari ya kutembelea kwa bei tofauti, yakiwamo ya chini ya Sh milioni 10 na mengine ya zaidi ya Sh milioni 20.

“Lakini nina wachungaji wa ngazi mbalimbali, hawa ni wale wa juu, wengine wachungaji wadogo wapo zaidi ya 670, hawa ni watenda kazi muhimu na wanatofautiana kwa ngazi zao, ndiyo maana kazi ya Mungu inasonga mbele hata nisipokuwapo,” alisema.

Mbali na magari ya wachungaji, pia amenunua mabasi 20 ya kubeba waumini kutoka na kwenda kanisani, yakianzia maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Alithibitisha kuwa, kila moja limegharimu kati ya Sh milioni 80 na 100. Mbali ya Mchungaji Gwajima, viongozi wengine wa makanisa wanaotajwa kuwa na utajiri mkubwa wa mali na fedha ni Nabii na Mtume Josephat Mwingira wa Kanisa la Efatha anayemiliki benki, mashamba makubwa na mali nyingine, Mchungaji Getrude Lwakatare wa Mikocheni B Assemblies of God anayemiliki mtandao wa shule za St. Mary’s nchini.

Wengine ni Askofu Zachary Kakobe wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship, Anthony Lusekelo `Mzee wa Upako’ wa Kanisa la Maombezi `GRC’ na Mtume Onesmo Ndegi wa Kanisa la Living Water Center ‘Makuti Kawe’.

- Habari Leo -