Advertise Here

Saturday, March 8, 2014

Rais Uhuru Kenyatta avutiwa na Uimbaji wa Rufftone.

kenyaatta
Rais Uhuru Kenyatta
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta ambaye siku chache zilizopita ameonesha nia yake ya wazi wazi ya kuutangaza zaidi Muziki wa Kenya, amekiri kuwa anapenda sana Mwimbaji wa nyimbo za Injili nchini humo Rufftone.

Kupitia mahojiano yaliyofanywa na Easy Fm, Katibu wa Mawasiliano na msemaji wa Rais wa Kenya Manoah Esipisu amesema kuwa Rais Kenyatta anaupenda sana Muziki wa Kenya, na kuwa Rufftone ndiye Mwimbaji anayempenda zaidi.

Rufftone ni moja mojawapo kubwa sana Nchini Kenya kwenye tasnia ya Muziki wa Injili, ambaye anafanya vizuri sana kwa sasa kupitia Wimbo wake wa "Mungu Baba" ambao alipata fursa ya kuuimba wakati wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya. Huku Kaka yake Daddy Owen akiendelea kufanya vizuri pia katika tasnia ya Muziki wa Injili Nchini Kenya.

Friday, March 7, 2014

Askofu Zygmunt Zimowski azindua mradi wa kupima na tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi Mkoani Shinyanga.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, hivi karibuni, alizindua mradi wa kupima na tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi, Jimbo Katoliki Shinyanga, Tanzania.

Ni mradi unaoendeshwa kati ya Mfuko wa Msamaria mwema, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Kampuni ya dawa kutoka Marekani ijulikanayo kama Gilead Sciences.

Zaidi ya watu 120, 000 wanatarajiwa kufaidika na mradi huu inayojikita katika: sheria na kanuni za tiba; maadili na utu wema. Watoto yatima watapewa kipaumbele cha pekee.

Mradi huu ni kielelezo cha mshikakano wa dhati katika mchakato wa kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili unaofanywa na Makanisa mahalia kama sehemu ya Uinjilishaji wa kina. Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya linapenda kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Jimbo Katoliki la Shinyanga.

Hizi ni juhudi zilizofanywa kwa ushirikiano mkubwa kati ya Marehemu Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki Shinyanga pamoja na Monsinyo Jean Marie Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, ambaye mara kadhaa alitembelea Tanzania ili kuangalia uwezekano wa utekelezaji wa mradi huu kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wa Ukimwi nchini Tanzania.

- Radio Vaticana -