Advertise Here

Saturday, March 8, 2014

Rais Uhuru Kenyatta avutiwa na Uimbaji wa Rufftone.

kenyaatta
Rais Uhuru Kenyatta
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta ambaye siku chache zilizopita ameonesha nia yake ya wazi wazi ya kuutangaza zaidi Muziki wa Kenya, amekiri kuwa anapenda sana Mwimbaji wa nyimbo za Injili nchini humo Rufftone.

Kupitia mahojiano yaliyofanywa na Easy Fm, Katibu wa Mawasiliano na msemaji wa Rais wa Kenya Manoah Esipisu amesema kuwa Rais Kenyatta anaupenda sana Muziki wa Kenya, na kuwa Rufftone ndiye Mwimbaji anayempenda zaidi.

Rufftone ni moja mojawapo kubwa sana Nchini Kenya kwenye tasnia ya Muziki wa Injili, ambaye anafanya vizuri sana kwa sasa kupitia Wimbo wake wa "Mungu Baba" ambao alipata fursa ya kuuimba wakati wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya. Huku Kaka yake Daddy Owen akiendelea kufanya vizuri pia katika tasnia ya Muziki wa Injili Nchini Kenya.

Friday, March 7, 2014

Askofu Zygmunt Zimowski azindua mradi wa kupima na tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi Mkoani Shinyanga.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, hivi karibuni, alizindua mradi wa kupima na tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi, Jimbo Katoliki Shinyanga, Tanzania.

Ni mradi unaoendeshwa kati ya Mfuko wa Msamaria mwema, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Kampuni ya dawa kutoka Marekani ijulikanayo kama Gilead Sciences.

Zaidi ya watu 120, 000 wanatarajiwa kufaidika na mradi huu inayojikita katika: sheria na kanuni za tiba; maadili na utu wema. Watoto yatima watapewa kipaumbele cha pekee.

Mradi huu ni kielelezo cha mshikakano wa dhati katika mchakato wa kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili unaofanywa na Makanisa mahalia kama sehemu ya Uinjilishaji wa kina. Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya linapenda kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Jimbo Katoliki la Shinyanga.

Hizi ni juhudi zilizofanywa kwa ushirikiano mkubwa kati ya Marehemu Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki Shinyanga pamoja na Monsinyo Jean Marie Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, ambaye mara kadhaa alitembelea Tanzania ili kuangalia uwezekano wa utekelezaji wa mradi huu kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wa Ukimwi nchini Tanzania.

- Radio Vaticana - 

Tuesday, February 25, 2014

Safu ya James Kalekwa: Mwisho tangu Mwanzo: Usuri wa njozi kwenye maisha binafsi Part 3


James Kalekwa
Kufuatilia sehemu ya pili ya somo Bofya Hapa

Njozi huweka boma au mipaka ya kieneo au aina ya watu unaopaswa kuwahudumia.
Ukiisoma vyema njozi ya mtume Paulo kwenye Matendo ya Mitume 26:15-18 ambayo yeye huiita “maono ya mbinguni” utagundua ya kwamba kuna aina fulani ya watu ambao Paulo anatumwa kwao, “… nikikuokoa na watu wako, na watu wa Mataifa, ambao nakutuma kwao…”  Wagalatia 2:7, “bali, kinyume cha hayo, walipoona ya kuwa nimekabidhiwa injili ya wasiotahiriwa, kama vile Petro ya waliotahiriwa.” Kutahiriwa na kutokutahiriwa ni lugha iliyotumika kueleza wayahudi (wanaotahiriwa) na watu wa mataifa (wasio tahiriwa)… Lugha ina mzizi toka kwenye agano la Mungu na Ibrahimu ambalo liliwekwa kwa tohara kwahiyo kutahiriwa kukawa ishara ya kuwa mtu yu katika agano na Mungu, Yehova. Kwahiyo mtume Paulo anapokea njozi maalum kwa ajili ya watu wa mataifa - hakuwa mtume kwa ajili ya watu wote!
Moyoni mwangu nilikuwa na maswali mengi sana ya kwamba ni kwanini Mungu anaachilia njozi ndani ya watu kwa ajili ya eneo fulani la kijiografia ama kwa ajili ya aina fulani ya watu? Wakati nikitafakari juu ya hayo ndipo ufahamu ukaniijia ya kwamba Mungu pekee ndiye Alfa na Omega; mwanzo na mwisho yaani hana mwanzo wala hana mwisho na pia Mungu yupo kila mahala kwa wakati mmoja (omnipresent). Lakini mwanadamu kwa asili anafungwa na hayo… Hawezi kuwepo kila mahala, kila wakati; hawezi kuwa kila kitu kwa kila mtu! Hivyo ni lazima mipaka hiyo iwe ndani ya njozi laasivyo njozi haitatimia… haitaufikilia mwisho wake!
Muhubiri 10:8 anasema mtu atakaye bomoa boma (boma la wakati na kijiografia ama asili fulani ya watu) nyoka atamwuma! Hebu tusome hii kwenye maandiko kisha tujifunze jambo katika mifano hiyo. Ndani ya kitabu cha Waamuzi sura ya 13 mpaka sura ya 16 kuna habari ya ndugu mmoja anaitwa Samsoni ambaye Biblia inamweleza kama mnadhiri wa Mungu. Ukisoma utaona jinsi Roho wa Mungu alivyokuwa akimshukia kwa nguvu… nguvu za kimwili kwasababu kusudi la kuzaliwa kwake lilikuwa ni kuwakomboa waisraeli kutoka kwenye uonevu wa Wafilsiti; kwahiyo ilikuwa ni sababu ya kivita hivyo alizihitaji nguvu hizo Waamuzi 13:5, “Kwani tazama, utachukua mimba, nawe utamzaa mtoto mwanaume; na wembe usipite juu ya kichwa chake; maana mtoto huyo atakuwa mnadhiri wa Mungu tangu tumboni; naye ataanza kuwaokoa Israeli na mikono ya Wafilisti.”. Hapo nimetamani uone kutoka kwenye maandiko jinsi malaika alivyoeleza lengo la kuzaliwa Samsoni. Kusudi lililonyuma ya kuzaliwa na kuishi kwa Samsoni… Hiyo ndiyo ilikuwa njozi ya maisha yake binafsi iliyounganikana na maisha ya taifa lake! 


Ukisoma habari zake kwenye sura nilizozitaja hapo juu utagundua kuwa karibia mara zote Samsoni alizitumia nguvu zake kutetea mahusiano (mapenzi) yake… Basi! Na mbaya zaidi ni kwamba Samsoni alienda kuoa nje ya taifa la Israeli kwahiyo alipokuwa anatumia nguvu zake kutetea mahusiano yake alikuwa ni nje ya kusudi la kuzaliwa kwake (out of scope). Alikuwa anatumia kitu sahihi kufanya kitu kisicho sahihi… Alitumia nguvu alizopewa na Mungu kuwapiga maadui wa taifa la Israeli; lakini kilichomsukuma kupigana na maadui haikuwa ni ukombozi wa taifa. Kwa maana nyingine ni kwamba mahusiano ilikuwa ni mlango wa kutokea (exit door) wa Samsoni na bila kujua alijikuta yuko nje ya boma. Alianza kupigana kukomboa mahusiano yake na kumbe Mungu alimkusudia apigane kuwaokoa Israeli na mikono ya Wafilisti. Hivyo alitumia nguvu nyingi sana lakini nje ya boma. Mwisho wake ulikuwa ni kutobolewa macho na kuteswa na Wafilisti kwa kupanga njama na mkewe Delila. Samsoni alikufa kifo cha kimasikini sana (alikufa akiwa mtumwa, akiwa ametobolewa macho, pasipo kutimiza ukombozi aliokusudia Mungu)! Alienda nje ya mipaka, alienda nje ya boma, alienda nje ya “scope” ya njozi yake. Kanuni inasema “…na mwenye kubomoa boma, nyoka atamwuma.”


Kuna mtumishi mmoja wa Mungu alitoa ushuhuda ambao uliyagusa maisha yangu sana. Ndugu huyo ameitwa na Mungu kufundisha neno la Mungu kwa watoto wa Mungu ili wakue katika kumjua Mungu na ameitwa maalum kwa ajili ya watu wa taifa husika barani Afrika. Udhihirsho wa Mungu ni mkubwa katika mafundisho yake! Watu wa nchi moja ya Amerika ya Kaskazini wakapenda sana huduma yake na wakatamani sana kufanya naye kazi ya Mungu. Wao walimuandalia kanisa kulea kama mchungaji wa kanisa la mahala husika na kuwa askofu wa hilo dhehebu. Walimwandalia malipo mazuri, nyumba nzuri na uhakika wa watoto wake kusoma, angepata huduma za afya, bima n.k (social security). Lakini jibu la yule mtumishi wa Mungu wa nchi ya Afrika ni kwamba angeenda kuhudumu nao wale watumishi, angekuwa nje wa “boma” la wito wa huduma yake. Angekuwa nje ya kusudi/njozi ya utumishi alioitiwa… Asingekuwa mwalimu wa neno la Mungu kama alivyo Afrika, kule angekuwa mchungaji na askofu na angekuwa mbali na watu alioitiwa kuwafundisha. Kama Paulo alivyoitwa kwa ajili ya watu wa mataifa, mtumishi yule aliitwa kwa ajili ya watu wa taifa lake la Kiafrika! Angebomoa boma la njozi yake… Nini kingetokea? “…na mwenye kubomoa boma, nyoka atamwuma.” Nilijifunza jambo la msingi sana kuhusu njozi katika ushuhuda huu. Watu wengi wangeweza kutoa visingizio kuwa “si unajua Mungu ni yule yule… si unajua kote, Amerika na Afrika, ni shambani mwa Bwana?... Si andiko limetuagiza twende ulimwenguni mwote?”. Kumbuka nilichokufundisha juu ya mipaka imbatanayo na njozi… Huwezi kuwa kila mahala kwa wakati mmoja, huwezi kuwa kila kitu kwa wakati mmoja na huwezi kuwepo milele hapa duniani. Visingizio vyote hivyo, tena ndugu wengine hutumia maandiko kuhalalisha utovu wa kinidhamu juu ya njozi (manipulation). Lakini hiyo haizuii ukweli kwamba nje ya boma ni kutafuta “kutobolewa macho.” Mungu akusaidie kuelewa jambo hili muhimu sana!

Somo hili litaendelea Jumatatu ijayo
Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa neno la Mungu. 
+255 714 762 669
+255 754 917 764
jameskalekwa@gmail.com

Mfahamu kiundani Mwimbaji Neema Decoras kutoka Tanzania.

Neema Decoras
Neema Decoras (Amezaliwa Tarehe 27 Julai 1984) ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo za Injili za Kikristo mwenye kipawa na hodari kutoka nchini Tanzania ambaye amejitoa kuwa chombo imara cha Uinjilisti na kutumikia kusudi la Mungu katika wakati wake. Alizaliwa katika jiji la Mbeya, Tanzania na ni watatu kuzaliwa katika familia ya watoto saba.

Neema Decoras ambaye kwa sasa ni mama wa watoto wawili wa kike na mke mpendwa wa mume mmoja alianza uimbaji wa nyimbo za injili akiwa mdogo sana katika shule ya Jumapili ya Kanisa La Pentekoste Tanzania (KLPT) kabla ya kuokoka na kubatizwa na mchungaji Mwakanyamale wa Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT) ya Ilembo, Airport, Mbeya.

Neema Decoras aliendelea na huduma ya uimbaji katika kipindi chote alichokuwa akisoma, kuanzia shule ya msingi hadi sekondari. Akiwa anachukua elimu ya sekondari alikuwa mwanachama na mwalimu wa kwaya ya Christ's Ambassadors Students Fellowship Tanzania (CASFETA) katika shule yake na muimbaji wa nyimbo za kusifu na kuabudu katika kikundi cha kusifu na kuabudu na Kwaya ya Tumaini ya Kanisa La Pentekoste Tanzania (KLPT). Ni katika kipindi hicho ndipo alipoanza kuwa na haja ya kukitumia kipawa cha uimbaji na utunzi wa nyimbo na kufanya huduma ya uimbaji kama muimbaji wa kujitegemea.

Haja ya kuwa muimbaji wa kujitegemea ilianza kutimia mwishoni mwa mwaka wa 2012 Neema Decoras alipofanikiwa kurekodi wimbo wake uitwao “Mungu ni Mwema” katika studio iitwayo Twins Records iliyopo Riverside, Ubungo jijini Dar es Salaam chini ya mtayarishaji wa muziki aitwaye Gabriel Maulana.

Mnamo January mwaka wa 2013 mume wake alimpeleka kwa mtayarishaji wa muziki aitwaye Ambangile Mbwanji anayejulikana sana kama Amba ambaye ni mmiliki wa studio iitwayo Amba Records iliyoko Ukonga, Jijini Dar es Salaam, Tanzania.

Katika studio hiyo alifanikiwa kurekodi na kutoa albamu yake ya kwanza mwezi Julai mwaka wa 2013. Albamu hiyo iitwayo “Milele Nitalisifu Jina Lako” ina nyimbo nane ambazo zote ameziimba kwa lugha ya Kiswahili. Nyimbo zilizomo katika albamu hiyo ni; Milele Nitalisifu Jina Lako, Mikononi mwa Mungu, Unapojaribiwa, Nione Leo, Mungu ni Mwema, Rejea kwa Yesu, Ninaimba Sifa na Hakika Nimejua.

Akiongozwa na Neno kutoka katika Zaburi 145:1-2 “Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, Nitalihimidi Jina lako milele na milele. Kila siku nitakuhimidi, Nitalisifu Jina Lako Milele na Milele” Neema Decoras anasema kamwe hawezi kuacha kulisifu Jina la Bwana kwa kuwa Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana.

Kwa sasa Neema Decoras anaishi jijini Dar es Salaam ambapo amefanya maonyesho yake mengi sana japo yuko tayari kutumika katika Ibada, Matamasha na Mikutano ya Injili, Semina, Sherehe, na matukio mbalimbali ambayo yanahubiri Neno la Mungu popote pale ndani na nje ya Tanzania.

Sikiliza Wimbo wake huu wa Milele Nitalisifu Jina lako Bwana
 

Wasiliana Nae Sasa
Simu: +255 658 027 515

Dini yazuia wananchi kwenda hospitali na sekondari.

DINI mpya iitwayo Matengenezo inayozuia waumini wake kwenda sekondari na hospitali, imeingia wilayani Kakonko mkoani Kigoma. Inakataza waumini wasiende sekondari na hospitali, kwa madai kuwa Biblia inawakataza kufanya hivyo. Mkuu wa Wilaya hiyo, Peter Toima alibaini hayo juzi katika Kijiji cha Rumashi Kata ya Nyabibuye wilayani humo.

Alikuwa kwenye ziara katika shule za sekondari za wilaya hiyo mpya, ambapo kwanza aligundua wanafunzi wengi hawajaripoti shuleni kuanza Kidato cha Kwanza.

Toima alipohoji kulikoni hawajaripoti katika shule walizopangiwa huku wale walioandikishwa darasa la kwanza, pia nao hawaripoti, alielezwa kuwa sababu za kiimani zinazokataza wengine kusoma.

Mkuu huyo wa Wilaya alikatiza ziara yake na kuanza msako wa kuwasaka wanafunzi hao ambao hawajaripoti shuleni pamoja na waumini wa dini hiyo ya Matengenezo.

Alisema aliamua kufanya hivyo, kwa sababu dini hiyo inawakosesha watoto haki yao ya msingi na kukiuka sheria za nchi, kwani ni haki ya kila mtoto kupata elimu.

Katika msako huo, aliongozana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo na watendaji wa Halmashauri wakiwemo Maofisa Elimu Msingi na Sekondari.

Viongozi hao walifika katika familia ya Mchungaji wa Kanisa la Matengenezo, Medad Laurent (40). Baada ya kufika hapo, Toima aliwakuta mabinti watatu waliochaguliwa kujiunga na Kidato cha Kwanza mwaka huu lakini hawajaenda, kutokana na kile Mchungaji huyo alichodai kuwa sekondari wanafundisha uongo, kinyume na maandiko matakatifu yanavyosema.

Kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Wilaya aliamuru Mchungaji huyo na mabinti zake wawili, kushikiliwa na Jeshi la Polisi huku utaratibu wa kuwapeleka mabinti hao shule ukiendelea. Pia, aliamuru Mchungaji huyo kuchukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria za elimu.

Siku iliyofuata Toima na Kamati ya Ulinzi na Usalama, walifanya kikao na kukubaliana kuwapeleka mabinti hao, Naomi Medard (16) na Anastazia Medard (14) katika shule za sekondari zenye mabweni kwa kuwatenganisha ili wasiendelee kusambaza sumu ya kukataa shule.

Naomi alipelekwa Shule ya Sekondari Nyamtukuza na Anastazia Shule ya Sekondari Kanyonza. Hata hivyo, katika familia hiyo binti mmoja Beatrice Merdad (19) alibaki nyumbani kwa madai kuwa hakuchaguliwa kuendelea na Kidato cha Kwanza.

Alidai kuwa hata angechaguliwa, asingeweza kuendelea kwani wanafundisha uongo na siku akifa hatakuwa na la kwenda kumwambia Muumba wake, kutokana na elimu hiyo ya dunia kuwapotosha.

Katika familia hiyo ya watoto saba, wawili walifariki dunia kutokana na kutokwenda hospitali. Mama wa watoto hao, Julitha Sebastian (39) alipohojiwa baada ya mtoto wake mchanga kuonekana kudhoofika na nywele kubadilika rangi, alisema kuwa dini yao haiwaruhusu kwenda hospitali.

Alisema hakuwahi kumpatia mtoto huyo chanjo ya aina yoyote wala hakuwahi kujifungulia hospitali. Kuhusu watoto wake waliokufa, alisema Biblia inasema “Ni heri wafao katika Bwana”.
Kaimu Ofisa Elimu Sekondari wa Wilaya hiyo, Florida Gandye alisema waumini wa kanisa hilo, awali walikuwa Wakristo Wasabato, kisha wakajiengua na kuanzisha dini hiyo yenye imani za ajabu.

- Habari Leo -

Mabomu yalipuka Makanisani.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi,Mkadam Khamis Mkadam
Watu  wanne wamejeruhiwa katika tukio moja kati ya manne ya milipuko ya mabomu yakiwamo mawili yaliyolipuka eneo la makanisa mawili visiwani hapa.

Katika tukio la kwanza, watu wanne walijeruhiwa baada ya mmoja wao kuokota mabaki ya silaha katika eneo la kufanyia mazoezi ya kijeshi huko Unguja Ukuu katika Wilaya ya Kusini Unguja.


Eneo hilo liko karibu na pwani na hutumiwa na wanajeshi kwa ajili ya kufanyia mazoezi.


Shabani Khamis Ibrahim, mmoja kati ya majeruhi wa tukio la Unguja Ukuu, aliyelazwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, aliliambia NIPASHE kuwa bomu hilo lililipuka akiwa kwa fundi akitengeneza pikipiki yake.


“Ghafla nilihisi kitu kimenipiga kiunoni na hapo ndipo nilipojihisi kuwa nimeumia na kukimbizwa hospitali,” alisema Shabani.


Majeruhi hao walifikishwa katika hospitali hiyo na watatu hali zao siyo nzuri ingawa mmoja ameruhusiwa.


Majeruhi hao ni Pandu Haji Pandu, Shabani Khamis Ibrahim, Juma Abdallah na Simai Hussein aliyeruhusiwa.


Matukio mengine ya milipuko ya mabomu yametokea katika makanisa mawili na katika mgahawa wa kitalii wa Mercury uliopo Forodhani.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, alithibitisha kutokea kwa matukio hayo juzi na jana na kwamba uchunguzi unaendelea.


“Tumefika eneo la matukio na ni kweli kuwa milipuko iliyotokea ni ya mabomu, ila bado hatujajua ni aina gani ya mabomu yaliotumika, hivyo ni mapema mno kusema kwani uchunguzi bado unaendelea,” alisema Kamanda Mkadam.


Matukio hayo yalitokea katika eneo la Mkunazini, Forodhani na Kijito Upele ambako hadi jana jioni hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na matukio hayo.


Mlipuko mwingine ulitokea karibu na Kanisa la Anglikana eneo la Mnara Mmoja saa 7:00 mchana.


Bomu hilo lilichimba barabara, ukuta wa kanisa hilo na kuvunja vioo vya gari moja lililokuwa limeegeshwa eneo hilo.


Mmiliki wa gari lililokuwa limeegeshwa, Mohamed Ibrahim Ali, alisema kuwa aliegesha gari lake eneo hilo na kwenda kuswali, lakini aliporejea na kukuta watu wakiwa wanashangaa mlipuko wa kwanza, aliingia katika gari laki na ghafla ulitokea mlipuko uliovunja vioo na kumsababishia michubuko.


Kamanda Mkadam alithibitisha kutokea kwa mlipuko huo, lakini alisema walichukua vipande vya mlipuko kwa ajili ya uchunguzi.

Vile vile, Kamanda Mkadam alisema juzi asubuhi ulitokea mlipuko nje ya Kanisa la Assemblies of God katika eneo la Kijito Upele, Wilaya ya Magharibi wakati waumini wakiendelea na ibada, lakini haukusababisha athari zozote.


Kuhusu mlipuko uliotokea katika mgahawa wa Mercury uliopo Forodhani, Kamanda Mkadam alisema lilitokea saa 6:00 mchana jana mbele ya mgahawa huo na kuchimba ardhini na kwamba wanaendelea na uchunguzi.

- Nipashe -

Saturday, February 22, 2014

Mwimbaji Sammie Okposo amzawadia gari Back Vocalist wake.

http://distilleryimage11.ak.instagram.com/fdbd8d4e9ac011e3916312179a3278fb_8.jpg
Kennedy akiwa na Gari yake Mpya
Mwimbaji wa Nyimbo za Injili nchini Nigeria Sammie Okposo amemstaajabisha back vocalist wake Kennedy Ogeleka kwa kumzawadia Gari Jipya kabisa aina ya Toyota Camry kwa kutumika nae kiaminifu kwa Miaka 8.
http://distilleryimage5.ak.instagram.com/d344e84c9abf11e3a60912ea6ba92f7d_8.jpg
Sammie (Kulia) akiwa na Kennedy
Akimkabidhi zawadi hiyo, Sammie alisema "Hongera sana Kennedy, Ninafuraha kuona nimeweza kuweka Tabasamu usoni kwako kwa kufanya kazi na mimi pamoja na bendi yangu kiuaminifu kwa Miaka 8. Ni maombi yangu kuwa Mazuri yote, Upendeleo, Kuongezeka na Baraka zikufuate wewe pamoja na kipawa chako.

Friday, February 21, 2014

Tazama Matokeo ya Kidato cha Nne ya Mtihani wa Mwaka 2013.

Matokeo ya Kidato cha Nne ya Mtihani uliofanywa Mwaka 2013 yametoka.

Kutazama Matokeo hayo Bofya Hapa Chini kwenye Kitufe
http://41.188.155.122/CSEE2013/olevel.htm

Taarifa kwa Umma kutoka Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste(PCT).

Rais wa Shirikisho la Muziki Tanzania Addo November akerwa na Wabunge wa Bunge la Katiba kutaka kuongezewa Posho.

Mwimbaji wa Nyimbo za Injili Tanzania ambaye pia ni Rais wa Shirikisho la Muziki Tanzania Addo November Mwasongwe, ameonyesha kuchukizwa na baadhi wa Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba kutaka kuongezewa Posho na kwamba Posho ya sasa Tshs. 300,000 haiwatoshi.

Addo November ameyasema hayo alipokuwa akiongea na Waandishi wa Habari Mkoani Arusha leo, na awataka Wajumbe wa Bunge hilo la Katiba wakumbuke kuwa Watanzania wamewaamini na ndio maana wako pale

Soma Status aliyoiandika Addo November kupitia Ukurasa wake wa Facebook

Thursday, February 20, 2014

Ikulu yatoa Majibu kuhusu Malalamiko ya Baraza la Maaskofu PCT kutoshiriki Bunge la Katiba.

ikulu picha
Baada ya kuwepo malalamiko toka kwa baraza la maaskofu wa kipentekoste Tanzania PCT kama taasisi rasmi kutopata ushiriki kwenye bunge la katiba la Tanzania ambalo limeanza wiki hii,Ofisi ya Rais wa jamhruri ya Muungano wa Tanzania imetoa taarifa rasmi ikiwa ni kujibu hoja iliyoibuliwa na baraza hilo siku chache zilizopita.

Ofisi ya Rais, Ikulu, imesema uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, haukuwa na nia ya kulibagua Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania,na kusema kua kuna kila sababu ya kuamini kuwa mapendekezo ya wajumbe kutoka baraza hilo hayakuwasilishwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi kama sheria ilivyohitaji. 

Pia, imesema pamoja na baraza hilo kutowasilisha mapendekezo yao kama ilivyotakiwa, litawakilishwa vyema na wajumbe walioteuliwa ambao wanajumuisha mjumbe aliyeteuliwa kutoka moja ya madhehebu yanayounda baraza hilo. 

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ikulu mjini Dar es Salaam, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk. Florence Turuka, alisema tamko la Baraza la Maaskofu kuwa linabaguliwa na serikali halina ukweli wowote. 

Dk. Turuka alitoa ufafanuzi huo kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, na kuongeza kuwa kama mapendekezo ya baraza hilo yengewasilishwa kwa mujibu wa sheria, yasingeachwa. 

Alisema uchunguzi uliofanywa na Ikulu, haujathibitisha kuwa baraza hilo liliwasilisha mapendekezo yake na kwamba ni vyema baraza likajiuliza kwanini kama kulikuwa na mapendekezo hayakufikishwa kwa wakati kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi, Zanzibar. 

Dk. Turuka, alisema iwapo mapendekezo ya baraza hilo yangefikishwa kwa makatibu wakuu hao, Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk. Alli Mohammed Sheni, wangechagua mwakilishi kutokana na mapendekezo hayo. 

Alisema uchambuzi wa majina ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba umebaini kati ya wajumbe 13 kutoka taasisi za kidini wa Tanzania Bara walioteuliwa, Respa Adam, ameteuliwa kutoka Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT), Patmos Vission, Kigamboni, ni moja ya madhehebu ambayo maaskofu wake wakuu wanaunda baraza hilo. 

Kwa mujibu wa Dk. Turuka, Februari 11, mwaka huu, baraza hilo lilitoa taarifa kwa vyombo vya habari kuwa limebaguliwa na serikali wanayoiheshimu, kuiombea na kuipenda katika uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba. 

Alisema anawahakikishia Watanzania hususan waliolengwa na taarifa ya baraza hilo kwamba serikali haikupuuzia kundi lolote lililoanishwa kwa mujibu wa sheria ya mabadiliko ya katiba.
Dk. Turuka alisema serikali inaliheshimu baraza na inalishukuru katika juhudi inazozifanya kwa kushirikina na serikali katika kuwaendeleza Watanzania.

Alisema makundi 850 yaliwasilisha mapendekezo ya majina 3,636, ambapo makundi ya kidini yalipendekeza majina 429. 
Katibu Mkuu huyo, alisema uchambuzi wa mapendekezo 52 yaliyowasilishwa nje ya muda, haukubaini kuwepo kwa mapendekezo kutoka baraza la maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.

- Mjap Inc -

Mpiganaji wa Ngumi wa Ghana Banku Ayitey atishia kumpiga TB Joshua.

Wednesday, February 19, 2014

Mchungaji afariki Dunia katika Mazingira ya kutatanisha nchini Kenya.

Mchungaji mmoja afariki Dunia huko Nairobi Kenya katika Mazingira ya Kutatanisha.

Tazama Video hii kwa Undani wa habari hii

Safu ya James Kalekwa; Mwisho tangu Mwanzo: Usuri wa njozi kwenye maisha binafsi. - Part 2

James Kalekwa
Msisitizo wa mwenendo wa somo:
Kusudi – ni sababu kuu ya kuwepo kwako. Hii hujibu swali la “Kwanini ninaishi?” mfano: Ninaishi ili kuudhihirisha utukufu wa Mungu kwenye kizazi changu.

Maono – ni taswira/picha kubwa uionayo juu ya mwisho wa maisha yako. Ni mkusanyiko wa mwisho wa maisha yako. Hii hujibu swali la “ninakwenda wapi?” mfano: … Kumtukuza Mungu kwa kufanya ugunduzi, uvumbuzi na utatuzi chanya wa mahitaji ya kizazi changu.

Dhamira – ni namna gani utafanya ili kuyafikia maono hayo kivitendo. Hii hujibu swali la “Namna gani nitatekeleza?” Mfano: … Kufungua taasisi ya utafiti wa uwezo wa mwanadamu na uelimishaji wa vijana.

N.B Unaweza kuwa na dhamira zaidi ya moja… Hakuna ukomo ilimradi tu dhamira zinafanikisha ufikiaji wa maono yako.

Malengo/Mipango – ni kuweka namna/njia za kivitendo na zinazopimika ili kufanikisha dhamira yako/zako Mfano: … Kufanya usajili wa taasisi yangu ifikapo March 28 ili kuanza utendaji rasmi.

Mkakati – ni mchanganuo wa hatua kwa hatua na uratibu wa rasilimali ili kufanikisha malengo yako. Hii hujibu maswali mengi “Nifanye nini, nifanye wapi, wakati gani?...” Mfano:

Taswira: Chombo cha Kusudi
Moyoni mwangu nimewiwa kuweka jambo hili kwa msisitizo mkubwa sana juu ya “Chombo cha kusudi”. Jifunze kutoka kwenye taswira hiyo na kutafsiri kwenye maisha yako binafsi.

Usuri ni nini?
Usuri (essence) ni jibu moja juu ya mjumuiko wa maswali mengi juu ya jambo, hoja, kitu au mtu fulani. Ni mara nyingi sana utawasikia watu wakitoa maelezo ya kina juu ya utumizi wa kifaa fulani cha umeme. Na kwa wanafunzi ni jambo lililozoeleka kukariri tafsiri (definition) na sifa za kitu au jambo fulani. Kuna aina ya watu ambao huvutika kufahamu sifa za kimwonekano za jambo fulani pasipo kujua tafsiri au utumizi wake.

Kwa ujumla wake, usuri hujibu maswali yahusianayo na maana na tafsiri ya jambo, sifa za kimwonekano, utumizi na huenda mbali na kujibu kwanini jambo fulani lipo na ni kwanini lipo vile lilivyo!
Kwahiyo, usuri wa maono si tafsiri/maana ya maono, si sifa za maono, si mwonekano na wala si utumizi wa maono…. Bali ni mjumuiko wa hayo yote! Karibu ujifunze kwa upana na urefu ujumla wa jambo hili muhimu sana katika maisha ya mwanadamu yeyote.

Njozi (Maono) huleta “mipaka” ya maisha
Ili kuupanua wigo wa kujifunza na kuvuta maarifa kutoka katika andiko hili, nitaleta tafsiri mbalimbali za lugha ya kiingereza na kuzitafsiri ili kutusaidia kupata upana wa maana ya hekima hizi.
“Where there is no revelation, people cast off restraint…”  (NIV)
“Where there is no prophetic vision the people cast off restraint…” (ESV)
Tafsiri yangu ya ujumla “Pasipo maono, watu hukosa/huvuka mipaka…”
Ukisoma kwenye historia ya agano la kale utaona kuwa miji mikubwa ilikuwa imezingirwa na kuta kubwa sana kuilinda miji hiyo; Mfano mji wa Yeriko, Yerusalemu. Hata kwenye historia ya kale, nchi kama China ya kale (Ancient China) utaona ujezi wa ukuta wa namna hiyo, ukuta mkuu wa China (The Great wall of China) ni moja kati ya kuta maarufu sana za miji.

Sababu kubwa ya ujenzi wa kuta hizo ilikuwa ni kuleta ulinzi wa uhakika kwa waishio ndani ya kuta hizo dhidi ya maadui walio nje ya kuta hizo. Ukuta uliweka mipaka baina ya walindwao dhidi ya wasiolindwa na ukuta huo; raia dhidi ya maadui wa jamii husika.

Mhubiri 10:8, “Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake; Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma.”
Njozi huweka bayana mipaka ya mtu ama jamii ibebayo njozi hiyo. Kimsingi, njozi kama ilivyo ni mipaka tayari. Njozi inaweka ukuta wa muda na wakati (season) ya kukamilika kwake, kwahiyo unapaswa kujua kuwa huna muda wote duniani kutimiliza njozi hiyo… Njozi imefungwa ndani ya muda. Kwenye kitabu changu cha kwanza nimeeleza kwa upana na kwa lugha nyepesi kuhusu sifa ya muda ya njozi. Njozi zote zina ukomo wa muda na kuna sababu katika hilo.
Ukisoma Habakuki 2:3, “ Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwakuwa haina budi kuja, haitakawia.” Utaona Mungu anasema na huyu ndugu kitu cha msingi sana juu ya “wakati ulioamriwa” na anasisitiza kuhusu mitazamo miwili; mtazamo wa kibinadamu na mtazamo wa kiMungu.

Kwamba katika macho ya kibinadamu njozi inaweza kuonekana inakawia lakini katika macho ya Mungu ipo katika wakati kwakuwa haina budi kuja. Hebu tazama hii sentensi ambayo Roho Mtakatifu aliweka kwa msisitizo sana ndani ya moyo wangu “…ijapokawia, ingojee; kwakuwa haina budi kuja, haitakawia.”.

Ukitazama utagundua hii ni kama sentensi yenye kujipinga yenyewe kwasababu inazungumza mawazo mawili tofauti yasiyoafikiana “… ijapokawia…. haitakawia”. Kitu gani ninataka uone katika eneo hili ni tofauti ya kutazama muda wa njozi iliyomo ndani ya mwanadamu na Mungu. Isaya 55:8-9, “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema BWANA. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu ya nchi.

Kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” Mungu anataka kusema namna ya kufikiri kwake ilivyo tofauti na juu ya namna yetu. Rejea Mhubiri 3:1, “Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” Na muendelezo wa mifano ya kila jambo na wakati wake mpaka mstari wa 8.

Somo hili litaendelea Jumatatu Ijayo
  
Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764

Sunday, February 16, 2014

Tazama wimbo wa Joepraize - Mighty God.

Namna Uzinduzi wa FRIENDS' BARBECUE(FB) ulivyofana Jijini Mwanza.

Ijumaa ya February 14, 2014 ilikuwa ni siku ya Uzinduzi wa Event ya FRIENDS' BARBECUE(FB) Mkoani Mwanza ambapo shughuli hiyo ilifanyika Royal Sunset Beach Resort maeneo ya Malimbe, Jijini Mwanza.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Maandalizi, Noel Mlabwa a.k.a Papaa alisema kuwa |Lengo hasa la kuanzisha FRIENDS' BARBECUE(FB) ni baada ya kuona Vijana wengi wa Kikristo hasa wa Jijini Mwanza hawana sehemu ya kwenda kufurahi kwa pamoja kama Vijana wa kipendwa, hivyo ujio wa Event hii utakuwa unawakutanisha Vijana na kupata Nyama Choma, Vinywaji, Mafundisho mbalimbali ya Kikristo hasa ya vijana na Live Music.

Siku ya tukio watu wengi walionekana kufurahia tukio huku wengine wakiomba tukio hilo liwe ni la Mara kwa Mara.

Sasa Tazama namna mambo yalivyokuwa
Noel Mlabwa akielezea Maana ya FRIENDS' BARBECUE na Umuhimu wake
Ma Mc wa Event hiyo Sowane Emmanuel na Kabula Siza
Ma Mc wakipata picha ya pamoja na Best Couple
Ufunguzi wa Shampein
Raha ya Shampein tuone mapovu
Shampein
Mc Kabula(Kushoto) akiwa na Muimbaji Ester Nyanda
Happy People
Ni zaidi ya Furaha
Best Couple ikipokea Zawadi yao
Bw. James Kalekwa akiwa eneo la tukio
Victoria Napiya(Kushoto) akiwa na Deborah Shija(Kulia) wakiwa na Furaha ya kutosha
Ester Nyanda akiimba
Papaa Noel Mlabwa akienda sawa wakati Ester Nyanda akiimba
Mazungumzo na Majadiliano
Papaa Noel akijibu baadhi ya Maswali kutoka kwa Mc
Baadhi ya waliohudhuria event hiyo wakiwa makini kufuatilia kilichokuwa kikiendelea
Bw. James Kalekwa akijibu Maswali kutoka kwa Mc
Deborah Shija akijibu Maswali kutoka kwa Mc
Kamati iliyoandaa Friends' Barbecue ikiimba wimbo Maalum
Mc Sowane Emmanuel akilonga Jambo
So Happy
Chakula kwa Tumbo, Tumbo kwa Chakula
Soft Music ikiendelea
Watu wakiendelea kula
Supu pia ilikuwepo
Mc Sowane na Lilian Mhando
Baadhi wa waliohudhuria
Ilikuwa ni Valentine Day
Very funny! Vick akinywa Shampein kwenye chupa


Wapo pia waliokuwa wakilia Jikoni

Hapo kila mtu alikuwa busy kupiga picha
Kaa tayari kwa FRIENDS' BARBECUE(FB) nyingine baada ya uzinduzi rasmi wa Event hiyo jijini Mwanza.