Advertise Here

Tuesday, December 10, 2013

Cheka na Mc Pilipili - Episode 3.

Leo ni Siku ya Jumanne na Kama kawaida siku ya Jumanne huwa tuna kitu kinaitwa "Cheka na Mc Pilipili".

Hivi unatambua kuwa Mc Pilipili ni Muhubiri na ni Mchungaji??? Sasa leo katika "Cheka na Mc Pilipili" tunakuletea moja ya Mafundisho ya Neno la Mungu ya Mc Pilipili, alipofundisha kupitia Kipindi cha Gospel Hits cha Sibuka Tv.

Haya Kazi kwako sasa kutazama

Monday, December 9, 2013

Mchungaji Gwajima kuhubiri Injili kwa Helikopta.

WAKATI viongozi wa madhehebu ya dini ya Kikristo nchini, wakionekana kushindana kwa utajiri, hali inayowafanya waishi `kifalme’ na kufungua miradi, Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amesema hana mpango wa kufungua biashara, zaidi ya kujikita na mahubiri ya Injili.

Aidha, amesema Mungu anaendelea kumbariki katika kazi yake, ndiyo maana mambo yake yanamnyookea, akitolea mfano kuwa baada ya kumiliki nyumba, magari na fedha za kutosha, sasa amembariki na kumpa helikopta atakayoitumia kufikia waumini wake wa ndani na nje ya nchi.

Usafiri huo wa angani, utaongeza idadi ya vyombo vya usafiri vya Mchungaji huyo, ambaye anatajwa kuongoza kwa utajiri miongoni mwa viongozi wa madhehebu ya Kikristo nchini, kwani anamiliki magari kadhaa, likiwamo lakifahari aina ya Hummer lenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 200.

Akizungumza na gazeti hili hivi karibuni kwa simu, Gwajima ambaye alikuwa anaendesha mikutano ya kueneza Neno la Mungu katika mikoa mbalimbali ikiwamo Kilimanjaro na Tanga, alisema helikopta imeshanunuliwa na matarajio yake ni kwamba, baada ya kukamilika taratibu zote za kisheria nchini, itawasili.

“Sipendi kusema mambo yangu sana, lakini kwa kuwa umeuliza naweza kugusia kidogo, ni kweli nina mpango wa kuanza kuhubiri Injili kwa helikopta, na kama ilivyo kwa gari, nayo hii nimepewa na watu wa Mungu walioguswa na huduma yangu Japan."

“Itafika nchini wakati wowote mambo ya kisheria yakikamilika, huu si wakati wa kuizungumzia sana maana bado haijafika,” alisema Gwajima ambaye gari lake aina ya Hummer liliwahi kuzua gumzo, wengine wakimhusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya, ingawa anapuuza madai hayo.

Mchungaji Gwajima, alieleza wazi kuwa utajiri wake unatokana na baraka anazopewa na anaowahudumia ndani na nje ya nchi na pia kazi yake ya kufundisha anayoifanya ughaibuni.

Aidha, kutokana na utajiri anaosema unatokana na baraka za Mungu, Mchungaji Gwajima anamiliki nyumba ya ghorofa nne eneo la Mbezi Beach katika Manispaa ya Kinondoni, ingawa haijakamilika.

Pia, amewanunulia wachungaji wake 40 magari ya kutembelea kwa bei tofauti, yakiwamo ya chini ya Sh milioni 10 na mengine ya zaidi ya Sh milioni 20.

“Lakini nina wachungaji wa ngazi mbalimbali, hawa ni wale wa juu, wengine wachungaji wadogo wapo zaidi ya 670, hawa ni watenda kazi muhimu na wanatofautiana kwa ngazi zao, ndiyo maana kazi ya Mungu inasonga mbele hata nisipokuwapo,” alisema.

Mbali na magari ya wachungaji, pia amenunua mabasi 20 ya kubeba waumini kutoka na kwenda kanisani, yakianzia maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Alithibitisha kuwa, kila moja limegharimu kati ya Sh milioni 80 na 100. Mbali ya Mchungaji Gwajima, viongozi wengine wa makanisa wanaotajwa kuwa na utajiri mkubwa wa mali na fedha ni Nabii na Mtume Josephat Mwingira wa Kanisa la Efatha anayemiliki benki, mashamba makubwa na mali nyingine, Mchungaji Getrude Lwakatare wa Mikocheni B Assemblies of God anayemiliki mtandao wa shule za St. Mary’s nchini.

Wengine ni Askofu Zachary Kakobe wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship, Anthony Lusekelo `Mzee wa Upako’ wa Kanisa la Maombezi `GRC’ na Mtume Onesmo Ndegi wa Kanisa la Living Water Center ‘Makuti Kawe’.

- Habari Leo -

Sunday, December 8, 2013

Viongozi wa Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani wamsifu Mzee Nelson Mandela.

Marehemu Nelson Mandela
Viongozi wakuu wa Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani katika salam zao za rambi rambi kwa wananchi wa Afrika ya Kusini, wamemsifu Mzee Nelson Mandela, aliyefariki dunia akiwa na umri wa miaka 95, kuwa ni kati ya watu walioacha mfano wa kuigwa kwa Jumuiya ya Kimataifa katika Karne ya ishirini na moja.

Ni kiongozi aliyesimamia kweli za maisha, akatetea haki na amani na kuhakikisha kwamba, demokrasi inapatikana na ubaguzi wa rangi unatokomezwa nchini Afrika ya Kusini. Ni kiongozi na mpigania haki ambaye alijikita zaidi katika majadiliano kama njia ya kufikia amani ya kweli badala ya kutumia silaha. Kwa miaka 27 akatupwa kizuizini, hadi alipoachiliwa huru kunako mwaka 1990, mchango mkubwa wa Kampeni ya Kimataifa. Mwaka 1993 akapewa tuzo ya amani duniani na kugawana na mpinzani wake Bwana Frederick W. de Klerk, watu ambao wameandika historia mpya ya Afrika ya Kusini.

Tata Madiba alipochaguliwa kuwaongoza wananchi wa Afrika ya Kusini, akataka kuona: utawala wa sheria na kwamba, ubaguzi wa rangi ulikuwa hauna tena nafasi kwa wananchi wa Afrika ya Kusini, bali wote kujitambua kwamba, ni wananchi wanaotegemeana na kusaidiana katika medani mbali mbali za maisha, kwa kuheshimu utu wa kila mtu na wala si rangi ya ngozi! Kila mtu akapata nafasi ya kushiriki maisha katika Afrika ya Kusini huru na mpya zaidi.

Kama Rais wa kwanza mzalendo, akagundua umuhimu wa upatanisho kama njia ya kuponya makovu ya chuki na ubaguzi wa rangi na kwamba, upatanisho ndiyo iliyokuwa njia pekee ya kudumisha misingi ya haki na amani ya kudumu. Watu wakapewa fursa ya kutubu na kuomba msamaha; ukweli ukafahamika na watu wakawa huru! Ndiyo maana watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaomboleza kwa kifo cha Mzee Madiba, mtu wa watu, liyeteseka kifungoni kwa miaka 27 na amevumilia pia mateso ya ugonjwa wake, hadi mauti yalipomfika hapo tarehe 5 Desemba 2013.

Hakuona kwamba uongozi ni kitu cha kung'ang'ania sana, akaamua kwa utashi wake kamili kung'atuka kutoka madarakani, viongozi wengine wakaendeleza pale aklipoachia Mzee Nelson Mandela. Apumzike kwa amani.

- Radio Vatican -

Mkutano wa Ufufuo na Uzima sasa kuhamia Morogoro.

Mch. Josephat Gwajima
Baada ya mikutano iliyovunja rekodi kwa idadi ya watu yaani Arusha, Moshi na Tanga; sasa kanisa la Ufufuo na Uzima linahamishia mikutano yake mkoani Morogoro ambapo Mchungaji Gwajima ambaye pia ni mchungaji kiongozi wa kanisa hilo anatarajiwa kuhubiri kwa siku nane mfululizo.

Pamoja Mchungaji Gwajima atafuatana na timi ya watendakazi zaidi ya mia tatu na waimbaji maarufu wa injili kama Flora Mbasha, John Lisu, Jackson Benty na Mwanamapinduzi Band.

Mkutano huo wa kwanza kufanyika Morogoro kwa kanisa la Ufufuo na Uzima unatarajiwa kushuhudia misukule wakirudi, wagonjwa kupona, viwete kutembea na mambo mengine mengi ya ajabu.

Usikose kuhudhuria na wewe ili kupokea muujiza wako.

- Ufufuo na Uzima -

Wednesday, December 4, 2013

Papa Francis adaiwa kutoroka Vatican usiku.

Papa Francis
Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis amedaiwa kutoroka usiku Makao Vatican ili apate fursa ya kwenda kutoa misaada kwa walemavu na watu wasiojiweza.

Tetesi za Papa Francis kuwatembelea maskini hao usiku kwa kujificha zimekuja baada ya mahojiano yaliyofanywa na Askofu Mkuu, Konrad Krajewski ambaye kazi yake kubwa ni kukusanya fedha toka kwa wasamaria wema na kuwapelekea maskini.

Imeelezwa kuwa Askofu Krajewski amekuwa akiambatana na Papa Francis wakati mwingine na kwenda kuwapa misaada maskini maeneo ya vijiji, mjini Vatican.

Askofu Krajewski alisema tangu zamani alipokuwa Askofu Mkuu wa Jimbo la Buenos Aires, Papa Francis amekuwa akipenda kwenda mijini nyakati za usiku na kuwatembelea wenye shida mbalimbali.

“Amekuwa akionyesha dalili ya kupenda kunisindikiza kwenda kuwapa misaada maskini, pindi nikiondoka kwenda kufanya kazi hiyo,” alisema Padri Krajewski.

Hata hivyo, alipoulizwa iwapo Papa aliwahi kwenda naye nje ya mji kwa ajili hiyo, Askofu Krajewski, alisita kujibu swali hilo.

Wakati huohuo, gazeti la Huffington Post limeripoti kuwa walinzi wa Uswisi, wamethibitisha kuwa Papa amekuwa akizunguka maeneo mbalimbali usiku akiwa amevalia mavazi ya kawaida ya wachungaji na kuwapa misaada, wanaume na wanawake wenye shida mbalimbali.

Tangu kuteuliwa kwake, papa Francis amevipamba vichwa vya habari duniani baada ya kuonekana akijaribu kuvaa kofia za polisi wa zimamoto, kuwaruhusu vijana wadogo wa kiume kuibusu miguu yake na kuwapigia simu waumini wake na kuzungumza nao.

Hivi karibuni, aliripotiwa katika vyombo vya habari akiwabusu na kuwafariji waumini walemavu katika Kanisa la Mtakatifu Peter, huku taarifa nyingine zikionyesha kuwa ametuma fedha zake binafsi kwa wahamiaji na wanaohangaikia mafao yao.

Alipokuwa Askofu Mkuu wa Jimbo la Buenos Aires, Papa Francis alifahamika kwa kutoroka usiku na kuwatafuta watu, kuzungumza nao na wakati mwingine kuwanunulia chakula.

Mapapa wengine waliopita pia wametajwa kutoroka usiku, kwa mfano papa John wa X111 alikuwa na tabia ya kutoroka usiku na kwenda mitaa ya Rome kufurahia uzuri wa jiji hilo, wakati Papa Pius wa X11 alivalia kama Mfaransa wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia na kwenda mipakani kuwasaidia Wayahudi wa Kirumi kisha kuwaweka katika sehemu salama.

- Mwananchi -

Tuesday, December 3, 2013

Daddy Owen kufunga ndoa mapema mwakani.

Daddy Owen. Photo-niaje
Daddy Owen
Mwimbaji Maarufu wa Muziki wa Injili toka Nchini Kenya Daddy Owen, ametangaza rasmi kufunga ndoa na Mchumba wake Fridah Wambui.

Daddy Owen amefikia Uamuzi huo baada ya kukamilisha taratibu zote za kimila, na kwasasa wanasubiri kupangwa kwa tarehe rasmi ya kufungwa kwa ndoa yao, huku akisema kuwa matarajio yao ni kufunga ndoa hiyo mapema Mwakani.

Monday, December 2, 2013

Tazama Video Mpya ya Mwimbaji Benjamin Dube.

Hii ni Video Mpya ya Wimbo wa Mwimbaji Benjamin Dube wa Afrika Kusini ujulikanao kama "Give Me Direction"

Friday, November 29, 2013

Waziri Mkuu aongoza Mazishi ya Askofu Simalenga.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Marehemu Askofu Simalenga
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda jana aliongoza mamia ya watu kwenye ibada ya maziko ya Askofu wa saba wa Dayosisi ya South West Tanganyika ya Kanisa la Anglikana nchini, Askofu John Simalenga iliyofanyika Njombe mjini.

Waziri Mkuu akiaga Mwili wa Marehemu
 Katika ibada hiyo iliyofanyika jana, Waziri Mkuu alisema Dayosisi imepoteza mhimili muhimu lakini akawataka wawe na umoja na upendo huku wakiendelea kumtumainia Mungu.

“Mhashamu Baba Askofu Simalenga alisimikwa Julai 6, 2008. Ni miaka mitano tu ya utumishi kwenu na alikuja wakati ambapo Dayosisi hii ilikuwa imekaa kwa miaka 10 bila ya kuwa na kiongozi. Siku anawekwa wakfu nilikuwepo na ninakumbuka mlimuomba asaidie kuleta mshikamano,” alisema Waziri Mkuu.
Ibada ikiendelea
 Aliendelea kusema, “Nawaomba wanadayosisi muwe na upendo na mshikamano mkubwa miongoni mwenu hadi hapo Mungu atakapotupatia kiongozi mwingine. Tumuombe Mungu ili kiongozi huyu ajaye apatikane kwa njia ya amani.

Alimuomba mke wa marehemu, Martha pamoja na watoto wa marehemu kupokea msiba huo kwa mikono miwili na kuahidi kuwaombea faraja kwa Mwenyezi Mungu.
Mwili wa Marehemu ukiwekwa Kaburini
Waziri Mkuu ambaye alishiriki maziko kwa niaba ya Serikali, alitumia fursa hiyo kuwapa pole maaskofu, mapadri, watawa na familia zikiwa ni salamu maalumu kutoka kwa Rais Jakaya Kikwete ambaye alisema yuko ziarani kwenye Mkoa mpya wa Simiyu.

Spika wa Bunge, Anne Makinda ambaye pia ni Mbunge wa Njombe Kusini ilipo Dayosisi hiyo, akitoa salamu za rambirambi alisema wana Njombe wamepungukiwa na nguvu kwa kuondokewa na kiongozi huyo wa dini.

“Alisaidia kuleta umoja hapa kwetu, tumempoteza mtu muhimu sana katika harakati za maendeleo ya wilaya yetu na mkoa kwa ujumla. Alisaidia kuleta umoja na upendo na sisi tuwe na upendo na amani, tuendelee kumuomba Mungu hadi tutakapoletewa msimamizi mwingine,” alisema Makinda.
Waziri Mkuu akiweka udongo katika Kaburi la Marehemu
 Katika mahubiri yake, Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Jacob Chimeledya alitaka waumini wote kumtazama Mungu na wamtegemee kwa sababu licha ya kwamba wanampenda askofu wao, ameona ni vema ampunzishe mtumishi wake.

“Sote tunajua kuwa katika kipindi chake, Dayosisi hii ilitulia kabisa je tutaruhusu kuondoka kwake kuzue tena chokochoko? Msiba huu usifike mahali ukaanza kututenganisha na kutoa mwanya wa kuanza kunyoosheana vidole. Tumuombe Mungu atusaidie afute machozi yetu,” alisema.

Askofu John Andrea Simalenga alizaliwa Novemba 30, 1953 na kufariki Novemba 24, 2013 baada ya kuugua kwa siku mbili. Novemba 22, mwaka huu alijisikia vibaya na alipopimwa alikutwa na malaria, kisukari na shinikizo la damu.

Alilazwa Hospitali ya Kibena, Njombe na kuruhusiwa siku iliyofuata lakini Novemba 24 alizidiwa tena na kuaga dunia. Ameacha mjane na watoto wanne.

- Habari Leo, Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu -

Thursday, November 28, 2013

Alichokiandika Rapper wa Muziki wa Injili Ulimwenguni Deitrick Haddon Juu ya Ujio wa Mtoto wake wa pili.

Mwimbaji Bernice Blackie wa Liberia kuzindua Video zake 8 kwa pamoja.

Bernice Blackie
Mwimbaji Bernice Blackie
Mwimbaji wa nyimbo za injili toka Liberia Bernice Blackie anatarajia kutoa Nyimbo 8 kwa pamoja katika Mfumo wa video, Desemba 8, Mwaka huu Uzinduzi utakaofanyika katika Kanisa la Providence Baptist Church.

Nyimbo hizo zilizo katika Mfumo wa Video zinatoka katika Album yake inayofanya vizuri kwasasa ya "You Na Do It Again".

Mbali ya Bernice kufanya Muziki wa Playback kwenye Matamasha mbalimbali kwa Miaka mingi, katika uzinduzi wa nyimbo hizo Bernice atafanya Live Performance, huku akisindikizwa na Waimbaji wengine kama Vivian Akoto, Sisters of Destiny, Christ Ambassadors, Pastor Clarke, na kundi maarufu la Philadelphia Dance group.

Waimbaji maarufu Nigeria wafunga ndoa.

Grace akiwa na Emmanuel
Waimbaji Maarufu wa Nyimbo za Injili nchini Nigeria Grace Okoduwa (Jahdiel) and  Emmanuel Benjamin (Eben) ambao wote ni washirika wa Kanisa la Christ Embassy, wamefunga ndoa ya asili Novemba 23 Mwaka huu, huku wakitarajia kufunga ndoa ya Kikristo Jumamosi hii ya Novemba 30 Mwaka huu.

Ndoa hiyo itafungwa katika Kanisa la Christ Embassy, na Itafungwa na Pastor Chris Oyakhilome, Mwanzilishi wa Kanisa hilo Ulimwenguni.

Grace Okoduwa (Jahdiel) anajulikana zaidi kwa wimbo wake maarufu ujulikanao kama "Heritage" na Emmanuel Benjamin (Eben) akijulikana zaidi kwa wimbo wa "Imaramma".

Hizi ni Picha za harusi yao ya Kiasili
Grace na Emmanuel
 
 
 
 
Tazama wimbo wa Jahdiel(Grace) Ujulikanao kama "Heritage"

Wednesday, November 27, 2013

Mwimbaji Solly Mahlangu wa Afrika Kusini kushiriki Tamasha la Chrismas.

Solly Mahlangu
MWIMBAJI Solly Mahlangu wa Afrika Kusini amekubali kutumbuiza kwenye Tamasha la Krismasi linaloandaliwa na Kampuni ya Msama Promotion ya Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurungenzi wa Msama Promotion, Alex Msama alisema mwimbaji huyo atakuja pamoja na waimbaji wake kwani anamiliki kikundi chake cha muziki wa Injili.

“Nashukuru maandalizi ya tamasha yanaendelea vizuri na naamini tamasha la mwaka huu litavutia kuliko yaliyotangulia kwani mwimbaji toka Afrika Kusini, Solly Mahlangu ambaye anaimba baadhi ya nyimbo zake kwa lugha ya Kiswahili amekubali kuja,” alisema Msama.

Baadhi ya nyimbo ambazo Solly Mahlangu ameimba kwa ludha ya Kiswahili ni Mwamba mwamba na Ee baba na zimewavutia waumini wengi hasa kwenye kuabudu.

Alisema ujumbe wa mwaka huu ni “Tanzania ni ya Watanzania, tutailinda na kuidumisha amani yetu.”

Msama alisema mwimbaji huyo anatarajia kushiriki katika tamasha hilo jijini Dar es Salaam, tamasha ambalo litafanyika pia katika mikoa ya Morogoro (Desemba 26), Tanga (Desemba 28), Arusha (Desemba 29) na Dodoma (Januari mosi).

Aidha, Msama alisema bado wanaendelea kufanya mazungumzo na waimbaji wengine yameshakamilika kwa waimbaji wa ndani na nje ya Tanzania ikiwa ni pamoja na Solomon Mukubwa (Kenya), Ephraim Sekeleti (Zambia), Liliane Kabaganza (Rwanda).

Waimbaji wa Tanzania ni pamoja na Rose Muhando, Upendo Nkone, Upendo Kilahiro, Edson Mwasabwite, New Life Band na John Lissu.

- Habari Leo -

Uzima wa Milele katika Damu ya Yesu Kristo - Mwl. Christopher Mwakasege (II).

Na Mwl. Christopher Mwakasege
- Inaendelea -

Yesu Kristo alisema ukiula mwili wake na kuinywa damu yake, yeye atakaa ndani yako na wewe utakaa ndani yake unapokea uzima wake wa milele unaokuvika tabia ya Uungu.

Haya ndiyo yaliyotokea kwa huyu mtoto mdogo wa umri wa miaka kumi na miwili. Huyu mtoto alipompokea Yesu Kristo na kuokoka – Kiroho aliula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake – akapokea uzima wa milele, Yesu Kristo aliingia ndani ya mtoto, na mtoto akaingia ndani ya Yesu Kristo – yote yalifanyika kwa Uwezo wa Roho Mtakatifu.

Unadhani mtoto huyu alipata wapi ujasiri wa kufanya sala yeye mwenyewe, kitu ambacho alikuwa anaogopa kufanya kabla hajaokoka?

Jibu lake ni – Damu ya Yesu Kristo! Imeandikwa hivi; “Basi ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu…….” (Waebrania 10:19).

Niliwahi kukaribishwa katika mkoa mwingine kuhubiri katika Kanisa fulani, nakumbuka kuwa nilihubiri juu ya Bartimayo yule kipofu aliyeponywa na Yesu Kristo kule Yeriko. Nilipomaliza mahubiri nilikaribisha watu waje mbele wale wanaotaka kuokoka na kuombewa magonjwa. Watu wengi waliokoka na pia kuponywa maradhi yaliyokuwa yanawasumbua.

Baada ya wiki moja kupita, alikuja mtu mmoja nyumbani kwangu tukasalimiana na nikamkaribisha aingie ndani. Alipokwisha kukaa kwenye kiti, akaniuliza akasema; “ Mlimpa kitu gani ndugu (alitaja jina lake) siku mlipokuja kuhubiri kanisani kwetu – maana mimi sikuwepo.

Nikamuuliza, “Kwani kumetokea nini?
Yule mgeni akasema; “Huyo ndugu alikuwa hawezi kunywa chai ya maziwa wala maziwa – akinywa maziwa alikuwa anaugua. Nilishangaa siku moja alifika nyumbani, nilipomkaribisha chai ya rangi alikataa, akasema sasa anakunywa chai ya maziwa bila shida yoyote.

Nilipomuuliza ameanza lini kunywa chai ya maziwa, akasema tangu baada ya maombi ya Jumapili pale Kanisani. Lakini pia, niliona tabia yake imebadilika. Alikuwa hachani nywele- sasa anachana. Alikuwa mlevi sana – sasa haonji tena pombe. Alikuwa mchafu, hajijali – nilishangaa kumwona amevaa nguo safi. Ni kitu gani mlimpa?

Nikamjibu nikasema; “ Sisi tulichokifanya ni kuhubiri habari za Yesu Kristo na uwezo wake. Ndugu yako alifungua moyo wake siku ile, akampokea Yesu Kristo moyoni mwake ili awe Bwana na Mwokozi wake akaokoka. Pia tukamuombea tatizo la ugonjwa alilokuwa nalo na Bwana akamponya”.

Ni jambo la kumsifu Mungu sana katika Kristo, kwa sababu baada ya huyo ndugu kuokoka, na maisha yake kubadilika – sasa hivi ana kazi nzuri ya kuajiriwa na pia, ni mhubiri wa injili. Jina la Bwana libarikiwe!

Huwezi ukampokea Yesu Kristo moyoni mwako na bado ukawa na tabia uliyokuwa nayo zamani. Unapompokea Yesu Kristo moyoni mwako – unapokea Uzima wa milele unaokupa tabia ya Uungu.
Yesu Kristo alisema hivi; “ Amini, amini, nawaambieni, msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake hamna Uzima ndani yenu…..Aulaye mwili wangu na kuinywa DAMU YANGU hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa pekee yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lolote…….Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa” (Yohana 6:53,56; Yohana 15:4,5,7)

Mtume Paulo alisema; “ Hata imekuwa, mtu akiwa NDANI YA KRISTO amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! Yamekuwa mapya” (2 Wakorintho 5:17).

Mtume Paulo alisema hivi katika waraka wake wa pili kwa watu wote, sura ya kwanza mstari wa tatu na wa nne; “Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima wa utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo atumetukirimia ahadi kubwa mno, za THAMANI, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa WASHIRIKA WA TABIA YA UUNGU, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa”.

- Mwisho -

Tuesday, November 26, 2013

Hawa ndio Wachungaji Watano Matajiri Nchini Nigeria.

Bishop David Oyedepo
1. Bishop David Oyedepo
Ni mwanzilishi wa Huduma ya "Living Faith World Outreach Ministry" maarufu kama Winners Chapel. Anaamika kuwa na Utajiri wa Dolla za Kimarekani 150. Alianzisha kanisani hilo Mwaka 1981, na kuanzia hapo likaanza kukua na kuwa Kanisa lenye waumini wengi sana Nchini Nigeria.

Bishop Oyedepo anamiliki ndege 4 binafsi na ana Makazi London na Marekani. Ni mwandishi wa Vitabu na pia anamiliki Kampuni ya Uchapishaji ijulikanayo kama Dominion Publishing. Mbali ya hayo, pia ana miliki Chuo Kikuu kijulikanacho kama Covenant University, Shule ya Faith Academy na Elite High School.


Richest Pastors
2. Chris Oyakhilome
Ni mwanzilishi wa Huduma ya "Believers' Loveworld Ministries" maarufu kama Christ Embassy. Ana utajiri kati ya Dolla za kimarekani Millioni 30 - Millioni 50. Kanisa lake lina Washirika zaidi ya Elfu Arobaini(40,000).

Anamiliki Kituo cha Luninga, Magazeti, Majarida, Hotel, na mengineyo. Kanisa lake lina Matawi Nigeria, Afrika Kusini, London, Canada, na Marekani. Kituo chake ca Luninga ndiyo kinachoamika kuwa kituo cha Kwanza cha Kikristo kurusha Matangazo yake Afrika Nzima kwa Masaa 24.

nigeria
3. Temitope Balogun Joshua (TB Joshua)
Ni mwanzilishi wa Kanisa la "Synagogue Church of All Nations (SCOAN)". Inaaminika kuwa ana utajiri wa dolla za Kimarekani kati ya Millioni 10 - Millioni 15. Alianzisha Kanisa hilo Mwaka 1987, na kwasasa ana Waumini zaidi ya Elfu Kumi na Tano(15,000).

Kanisa lake lina Matawi ghana, UK, Afrika Kusini na Ugiriki. Kwa miaka kadhaa iliyopita, TB Joshua ameweza kuchangia huduma mbalimbali kama vile Elimu, Afya na Huduma za Matengenezo mbalimbali kwa zaidi ya Dolla za kimarekani Millioni 20. Ana miliki pia Kituo cha Luninga cha Emmanuel Tv.


Matthew Ashimolowo Net Worth
4. Matthew Ashimolowo
Ni mwanzilishi wa Kanisa la "Kingsway International Christian Centre (KICC)". Anatajwa kuwa na Utajiri wa Dolla za Kimarekani kati la Millioni 6 - Millioni 10. Mwaka 1992 alitumwa na Kanisa lake la awali la "Foursquare Gospel Church" la Nchini Nigeria kwenda kufungua tawi London, na badala yake akafungua Kanisa lake la "Kingsway International Christian Centre (KICC)" ambalo ni Moja ya Kanisa Kubwa sana huko UK.

Mshahara wake kwa Mwaka Mmoja ni Dolla za Kimarekani Laki 2(200,000) na Kiasi cha Utajiri wake mwingine kinatoka kwenye biashara anazofanya ikiwa ni pamoja na kampuni yake inayoandaa Makala mbalimbali za kikristo.


Chris Okotie Net Worth
5. Chris Okotie
Ni mwanzilishi wa Kanisa la "Household of God Church". Okotie alikuwa Mwanamuziki wa Pop miaka iliyopita na baadaye aliamua kuokoka na kuwa Muhubiri baada ya Miaka kadhaa.

Kanisa lake linakadiriwa kuwa na Waumini Elfu Tano(5,000) ambao wengi wao ni Watu maarufu wa Nigeria kama wanamuziki. Amegombea Urais wa Nigeria mara tatu na hakufanikiwa kushinda hata mara moja.

Orodha hii ni kwa Mujibu wa Mtandao wa "Celebrity Networth" iliyotolewa Mwezi wa 8, Mwaka huu.

Cheka na Mc Pilipili - Episode 2.

Leo ni Jumanne na kama kawaida kila Jumanne kupitia Mtandao huu, tunakuletea "Cheka na Mc Pilipili" ikiwa ni vichekesho ambavyo amevifanya Mc Pilipili katika Maeneo mbalimbali.

Sasa leo Mc Pilipili anatukumbusha enzi za shule Msingi mambo yalivyokuwa. Je! Wewe unakumbuka enzi za shule ya Msingi mambo yalikuwaje??? Tazama Video hii uvunje mbavu zako

Monday, November 25, 2013

Mwimbaji Enid Moraa wa Kenya afiwa na Baba yake.

enid moraa dad
Enid akiwa na Baba yake enzi za Uhai wake (Picha na Uliza Links)
Mwimbaji wa nyimbo za Injili wa Nchini Kenya Enid Moraa amefiwa na Baba yake Mr. David Onkoba Nyakundi baada ya kulazwa katika Hospitali ya Aghakhan toka Septemba 22, 2013 katika chumba cha ICU.

Baba yake Enid alipelekwa hospitali hapo akiwa na Matatizo katika Mwili wake yaliyosababishwa na kinachoitwa "Electrolyte Imbalance".

Amani ya Bwana ipitayo akili za Mwanadamu iwe na Familia hii katika kipindi hiki kigumu.

Kwa mara ya kwanza Papa Francis aonesha Mabaki ya Mtakatifu Petro.

Waumini wa Kanisa Katoliki duniani wameoneshwa kwa mara ya kwanza mabaki  ya Mtakatifu Petro toka kupatikana kwake Miaka ya 1940.

Mabaki hayo ya Mtakatifu Petro, yalioneshwa kwa waumini hao huku yakiwa yamewekwa katika kisanduku katika misa  iliyo ongozwa na Papa Fransisco jumapili ya Jana.


Kuoneshwa kwa mabaki hayo kwa waumini wa kanisa Katoliki inaaminika kutaongeza Imani ya waumini wa kanisa hilo, hasa baada ya kukumbwa na  mikasa ya utovu wa nidhamu ya kimaadili kwa wafanyakazi na wahudumu wa kanisa hilo katika sehemu tofauti duniani.

Tazama Video hii ya Papa Francisco akionesha Mabaki hayo

- Kwa Msaada wa Launite Blog -

Askofu Simalenga afariki Dunia.

Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kusini Magharibi mwa Tanganyika, Jimbo la Njombe, John Simalenga (60), amefariki
ghafla akiwa nyumbani kwake Njombe, Mkoa Mpya wa Njombe, baada ya kuugua kwa muda mfupi.

 

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu Mkuu wa Kanisa hilo nchini, Dickson Chilongani alisema Askofu huyo alifariki jana saa 11 alfajiri baada ya kuugua malaria na kupelekwa katika Hospitali ya Dayosisi hiyo.

 

"Marehenu Askofu Simalenga siku moja kabla ya mauti, aliugua malaria na kupelekwa katika Hospitali ya Dayosisi, baada ya kupimwa aligundulika kuwa na kisukari pamoja na presha kuwa juu," alisema Chilongani.

 

Aliongeza kuwa, baada ya kufanyiwa vipimo aliruhusiwa kurudi nyumbani na kupewa dawa wakiamini zitamsaidia lakini hali yake ilibadilika ghafla na kufikwa na umauti.

 

Chilongani aliwataka Wakristo wote nchini, kuungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki kigumu ambapo taratibu za mazishi zinaendelea kufanyika.

 

Marehemu Askofu Simalenga alizaliwa Novemba 30,1953 katika Kijiji cha Milo, Wilaya Ludewa, mkoani Iringa. Alimaliza elimu ya msingi mwaka 1997 na 1971 alihitimu kidato cha nne.

 

Mwaka 1973 alihitimu kidato cha sita ambapo mwaka 1974-1977 alijiunga na Chuo Kikuu nchini Kenya na baadaye alienda nchini Uingereza kupata Shahada ya pili katika chuo cha Hull.

 

Amewahi kuwa Askofu Mkuu katika Kanisa la Mtakatifu Andrea Njombe, Mchungaji kiongozi Kanisa la Mtakatifu Albano, Dar es Salaam na kufundisha katika Chuo cha Mtakatifu Mark's.

 - Gazeti la Majira -

Yaliyojiri kwenye "Nataka Nimjue" ya Christina Shusho.

Christina Shusho
Kwa Mara ya Kwanza katika Historia ya Muziki wa Christina Shusho toka Tanzania, Jana ilikuwa ni Siku ya Live DVD Recording yake iliyofanyika pale City Christian Centre, Upanga Jijini Dar es salaam.

Watu wengi wamezoea kumuona Christina Shusho akiimba kwa Kutumia CD "Playback", lakini Jana aliudhihirishia Uma kuwa hata kuimba LIVE pia anaweza. Kazi hiyo kubwa imefanywa chini ya Music Director Samuel Yonah.

Katika tukio hilo, waimbaji mbalimbali walikuwepo kumsindikiza Christina Shusho kama vile Upendo Kilahiro, The Voice Acapella, na wengineo

Mambo yalikuwa hivi
Shusho On Stage
Backups wakienda sawa
Ilikuwa ni Shangwe na ndelemo
Hii ilikuwa ni Collabo kati ya Shusho na The Voice
Kila chombo kilikuwepo kuhakikisha Mungu anapewa Utukufu wa kutosha
Hiki ndo Kikosi kazi

- Picha zote na Uncle Jimmy -

Sunday, November 24, 2013

Kulola Junior na Frolian Katunzi watikisa Jiji la Mwanza.

Mkutano wa Injili ulioandaliwa na Kanisa la EAGT City Centre chini ya Mchungaji Michael G. Kulola(Kulola Junior) umeanza katika Viwanja vya Furahisha jijini Mwanza na utadumu kwa Siku 8.
Wanenaji katika mkutano huo ni Mchungaji Frolian Katunzi kutoka Dar es salaam, Mchungaji Frank Msuya toka Arusha na Mchungaji Michael Kulola toka Mwanza.
Kwaya mbalimbali pamoja na Waimbaji mbalimbali wanahudumu katika Mkutano huo kama vile Bugando Injili, City Centre Choir, Mlima wa Utukufu(Ilemela), Lusekelo kutoka Dar, na wengineo.

Mwanamuziki Kidumu aeleza sababu ya yeye kuchanganya Muziki wa Injili na wa Kidunia.

Kidumu
Mwanamuziki Kidumu mwenye asili ya Burundi aishiye Kenya ameelezea sababu zinazomfanya kuimba Muziki mchanganyiko yaani Muziki wa injili pamoja na Muziki wa Kidunia.

Kidumu amesema kuwa yeye si Mchungaji wala si Mwalimu wa Dini, ila yeye ni Msanii anayeishi kwa kufuata wito wa Mungu.

"Gospel ilivyo si kama watu wengi wanavyoifikiria. Msanii ni kioo cha Jamii, na kila ninalolifanya linafundisha jamii katika mambo yanayowaathiri sana. Daddy Owen alipoimba wimbo wa "Mbona" alikuwa akizungumzia namna watu wenye ulemavu wanavyonyanyapaliwa. Jamii inapaswa kuelimishwa kuhusu Magonjwa, Upendo, Amani, Ukabila, Siasa pamoja na mambo mengine yanayowagusa. Hicho ndicho ninachokifanya." Amesema Kidumu.

Anasema Wokovu si kuimba tu kuhusiana na Habari za kwenda Mbinguni, au kujaza Jina Yesu kwenye Mistari ya wimbo, bali pia ni Kutoa taarifa zenye manufaa kwa jamii.

Lifahamu kiundani Kundi la "Beyond Vocal" kutoka Afrika Kusini.

Beyond Vocal
Beyond Vocal ni kundi lenye Vijana Watano wanaoimba Muziki wa Injili. Kundi hili Maskani yake ni Nchini Afrika Kusini, na Staili ya Muziki wao ni wa kuimba pasipo kutumia chombo chochote cha muziki(yaani Acapella), huku "Beat" ikitengenezwa kwa Midomo tu.

Kwa hapa nyumbani Tanzania Kundi hili la Beyond Vocal tunaweza kulifananisha na Kundi la The Voice Acapella, ambao nao huwa wanafanya Muziki wa aina kama hii.

Kundi hili la Beyond Vocal lilianzishwa Mwaka 2008, na Waanzilishi wa kundi hili ni Alex Granger, Lisanse Changwe, Mduduzi Dlamini ,Willard Sibande na Scelo Mhlanga.

Mpaka sasa kundi hili lina Album mbili. Album yao ya Kwanza ilikuwa ni "Trust In The Lord" na Album ya Pili inajulikana kama "Hold On", Kazi iliyofanywa chini ya Record Lebel ya "Spirit Music".

Waimbaji katika kundi hilo wamekuwa wakija na wengine kutoka na mpaka sasa kundi hilo linaundwa na Scelo Mhlanga kama "Lead", Mduduzi Dlamini kama "Bassist", Mbuso Vundla kama "1st Tenor", Nkosana Msimang kama "2nd Tenor/Baritone/Vocal Percussion", na Ntako Mosia kama "Baritone".
Beyond Vocal katika pozi
Kundi hili limepata nafasi pia ya ku'perform kwenye Jukwaaa moja na Waimbaji nguli mbalimbali kama vile Benjamin Dube, Solly Mahlangu, Ernie Smith, Brenda Fassie, Tshepiso, Andile B, Mari Michael, the late Isaac Mthethwa, Nathi Zungu, Dr Gumbi, na wengine wengi.

Pia wameshafanya ziara za Kimuziki katika Nchi mbalimbali kama Swaziland, Botswana, Zimbabwe pamoja na nyumbani Afrika Kusini.

Malengo Makubwa ya kundi hili la Beyond Vocal ni kuwa Huduma inayobadili Maisha ya watu, kwao wenyewe lakini pia kwa watu wengine.

Sasa hebu Tazama Video hii, Beyond Vocal wakiimba "Live" wimbo wa "Ndixolele" katika Show ya "expresso"

Saturday, November 23, 2013

Mchungaji aapa kumlinda Mwanamuziki Justin Bieber.

Mchungaji Judah Smith(Kushoto) akiwa na Justin Bieber
Mchungaji mmoja wa Kanisa la "Washington-based City Church" Mchungaji Judah Smith amesema kuwa yupo tayari kumlinda Mwanamuziki Justin Bieber dhidi ya Vyombo vya habari zinavyomchafua Mwanamuziki huyo kila iitwapo leo.

Kauli ya Mchungaji Smith imekuja siku chache baada ya Ripota mmoja wa Hollywood kuandika Makala iliyodai kuwa Siku chache zilizopita Mwanamuziki huyo Justin Bieber alizini na Kahaba mmoja wa Kibrazili, huku Mchungaji Smith akidai kuwa Ripoti hiyo si ya kweli na ina lengo la kumchafua Justin Bieber.

Mchungaji Smith amemsihi Justin Bieber kutupilia mbali madai hayo na asonge mbele zaidi, huku akiwataka watu kumtazama justin Bieber katika Mtazamo mpana wa Mazuri anayoyafanya kuliko kumchafua kila siku.

Smith ambaye mara nyingi amekuwa akizungumza kwenye Vyombo vya Habari kwa niaba ya Justin Bieber, ni rafiki wa karibu wa Mama yake Justin Bieber ambaye walifahamiana naye Miaka mitatu iliyopita.

Katika kuhakikisha kuwa Justin Bieber anakaa kwenye Mstaari Mnyoofu wa Kimungu, Mchungaji Smith amekuwa akimtumia Mistari mbalimbali ya kwenye Biblia Justin Bieber kupitia Mitandao mbalimbali ya Kijamii.

"Nataka Nimjue" ya Christina Shusho Live Jumapili hii pale CCC.

Mwimbaji wa Nyimbo za Injili toka Nigeria Sammie Okposo atoa wimbo mpya.

Sammie Okposo
Mwimbaji maarufu wa nyimbo za Injili toka Nigeria Sammie Okposo ambaye ameshinda Tuzo ya Mwimbaji bora wa nyimbo za Injili Nigeria, ametoa wimbo wake wa kwanza kutoka kwenye Album yake mpya anayotarajia kuzindua rasmi Mwakani mwezi wa April.

Kwa mujibu wa maelezo yake, wimbo huo mtu akiusikiliza kwa mara ya kwanza, anaweza akahisi kama sio wimbo injili kwani una "beat" inayokwenda kasi sana, hivyo kuueewa inahitaji mtu atulie na asikilize ujumbe uliopo kwenye wimbo huo.

Wimbo huo unajulikana kama "Who Tell You Say?", huku Okposo akisema sasa ni wakati wa kupeleka Injili katika Kumbi mbalimbali za Starehe ambako Injili haihubiriwi.

Hapa anasema, "Ni muda sasa kuhubiri Injili katika kumbi mbalimbali za starehe maarufu kama "Clubs" na maeneo mengine ambako Injili haihubiriwi. Injili haitakiwi kuhubiriwa makanisani tu, mana kuna watu walio nje ya makanisa na wanahitaji kuhubiriwa Injili".

Kabla ya kuzindua Album yake hiyo, Okposo amepanga kutoa Nyimbo mbili zilizopo kwenye Album yake hiyo mpya.

Rais Vjekoslav Bevanda akutana na Papa Francisko mjini Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko, amekutana na kuzungumza na Bwana Vjekoslav Bevanda Novemba 22, 2013, ambaye ni Rais wa Baraza la Mawaziri nchini Bosnia na Erzegovina, ambaye pamoja na ujumbe wake amekutana na Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyeambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Mazungumzo haya ambayo yamefanyika katika hali ya urafiki, imekuwa ni fursa kwa viongozi hawa wawili kujadili pamoja na mambo mengine hali halisi ilivyo nchini Bosnia na Erxegovina sanjari na kuanzisha mchakato utakaoiwezesha nchi hii kuwa wazi zaidi kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu pamoja na changamoto za athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Pande zote mbili zimeridhika kwa uhusiano uliofikiwa kati ya pande hizi mbili, mintarafu itifaki ya mwaka 2006, ulioonesha umuhimu wa mshikamano na ushirikiano kati ya Kanisa na Serikali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Katika mazungumzo yao wameangalia pia jinsi ya kutekeleza itifaki hii na jinsi ambavyo Kanisa Katoliki linaweza kuchangia zaidi katika ustawi wa nchi yao.

- Radio Vatican -

Wimbo wa "Nitumezi" wa Bumie toka Zambia wafanya vizuri kwasasa.

Mwimbaji wa kike anayefanya vizuri Nchini Zambia Born Bunmi Dada a.k.a Bumie, Wimbo wake wa "Nitumezi" ukiwa na maana ya "Asante" unafanya vizuri sana kwasasa.

Bumie mwenye asili ya Lagos-Nigeria baada ya kukamilisha wimbo wa "Nitumezi", Wimbo huo umepata nafasi ya Kuchezwa sana kwenye Radio mbalimbali huko Zambia.

Album ya kwanza ya Bumie ilijulikana kama "My All" na ilitoka mwanzoni mwa huu. Kupitia Album hiyo, Bumie ameweza kupata mialiko mbalimbali ndani na nje ya Nchi ya Zambia, kama Marekani ambako alionekana kwenye Vipindi mbalimbali vya Runinga na Kusikika kwenye Radio.

Bumie anayesifika sana pia kwa Uzuri wake, pia ana sauti nzuri ambayo ameamua kuitumia katika Kumsifu Mungu.

Friday, November 22, 2013

Uchaguzi wa viongozi wapya Tafes Saut kufanyika kesho.

Noel Didas, Mwenyekiti anayemaliza muda wake
Jumamosi ya Kesho kutakuwa na Uchaguzi wa Viongozi wapya wa Tafes Saut-Mwanza. Uchaguzi huo utahusisha Viongozi wa Juu kama vile Mwenyekiti, Katibu, Muweka Hazina, n.k.

Uchaguzi huo utafanyika Saa 10:00 Jioni - Saa 12:30 Jioni, katika Ukumbi wa M1 ndani ya chuo Kikuu cha Mt. Augustino.

Tazama Video Mpya ya Mwimbaji Goodluck Gozbert.

Hii ndo Video Mpya ya Mwimbaji wa Nyimbo za Injili toka Mwanza, Tanzania anayejulikana kama Goodluck Gozbert. Wimbo Unajulikana kama "Umetamalaki" kazi iliyofanywa na Usanifu Experts Videoz.

Thursday, November 21, 2013

Elias Mwingira na Mkewe washerehekea Miaka 20 ya ndoa yao.

Nabii Josephat Mwingira akiwa na Mkewe Mchungaji Eliakunda Mwingira
Mtume na Nabii Josephat Elias Mwingira na Mkewe, Mchungaji Eliakunda Josephat Elias Mwingira, wanasherehekea Miaka 20 ya Ndoa yao.

Ibada maalum kwa ajili ya Sherehe hiyo, itafanyika Jumamosi ya November 23, 2013 katika Kanisa la Efatha Mwenge, Dar es Salaam.

Mwinjilisti wa Kimataifa Billy Graham alazwa hospitali kwa Matatizo ya Upumuaji.

Billy Graham
Billy Graham, siku ya birthday yake ya Kutimiza Miaka 95
Mwinjilisti wa kimataifa Billy Graham amelazwa katika Hospitali ya Asheville Jumanne ya Wiki hii baada ya kukumbwa na Matatizo katika Mfumo wake wa Upumuaji.

Graham ambaye ametimiza Miaka 95 Mwanzoni mwa Mwezi huu, anatarajiwa kuruhusiwa kurudi nyumbani siku yoyote kuanzia leo.

"Bw. Graham yuko hospitali akisumbuliwa na Matatizo ya Upumuaji, tatizo alilokuwa nalo pia wiki chache zilizopita. Hivyo tunatarajia ataruhusiwa wakati wowote ndani ya siku hizi mbili". Alisema Msemaji wa Graham.

Graham ambaye hakuwahi kuhubiri kwenye Umati wa watu kwa takribani Miaka 7, Sauti yake ilisikika tena katika birthday yake, akihubiri huku akiwa amerekodiwa.

Meya aokoka na kuachana na Ulevi na Madawa ya Kulevya.

Meya Rob Ford
Meya wa mji wa Toronto nchini Canada, Rob Ford, ameasi ulevi baada ya ‘kuokoka’. Jambo hili limetokea baada ya Makansela wa baraza la jiji kumpunguzia madaraka yake.

Bwana Rob Ford mwenye umri wa miaka 22 anasema ameamua kuasi pombe, baada ya kuokoka na kumtambua Yesu huku akisema kuwa kamwe hatawahi kuonja tone la pombe.

Kabla ya kumtambua Yesu, Bwana Rob aliahidi kuwapiga vita Makansela waliopiga kura kumpunguzia mamlaka.

Waziri mkuu wa Canada, Stephen Harper alisema kuwa madai dhidi ya Bwana Ford ni ya kusikitisha sana.

Meya huyo alikabiliwa na shinikizo kujiuzulu baada ya kukiri kuwa aliwahi kutumia dawa ya kulevya aina ya Cocaine wakati alipokuwa mlevi chakari.

Pia anakabiliwa na madai ya kumtongoza mfanyakazi wake mmoja wa kike pamoja na kutumia lugha chafu, kuwatisha wafanyakazi wake na kuwa na uhusiano wa kimapanzi na kahaba.

Kwenye mahojiano na moja ya vyombo vya habari nchini humo, Ford alisema hajaonja mvinyo kwa wiki tatu na kuwa hatawahi kamwe kunywa pombe.

"Nimeweza kumtambua Yesu kama mwokozi wangu.,’’ alisema Ford.

- BBC Swahili -

Wednesday, November 20, 2013

Uzima wa Milele katika Damu ya Yesu Kristo - Mwl. christopher Mwakasege (I).

Na Mwl. Christopher Mwakasege
“Basi Yesu akawaambia, Amini, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kunywa damu yake, hamna Uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao UZIMA WA MILELE; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli; na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi” (Yohana 6:53-57).

Mtu ambaye ameula mwili wa Kristo na kuinywa damu yake ile iliyomwagika msalabani, ni yule ambaye anakaa ndani ya Yesu Kristo, na Yesu Kristo anakaa ndani yake. Kwa maneno mengine amepokea uzima wa Mungu, ambao ni uzima wa milele. Unapompokea Yesu Kristo moyoni mwako unapokea uzima wa milele; kwa kuwa, “Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu” (Yohana 1:4).

Inatupasa tukumbuke ya kuwa, kwa mtu mmoja Adamu, dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.

Pia, inatupasa tukumbuke ya kuwa, “ikiwa kwa kukosa mtu mmoja mauti ilitawala kwa sababu ya yule mmoja, zaidi sana wao wapokeao wingi wa neema, na kile kipawa cha haki, watatawala katika UZIMA kwa yule mmoja, Yesu Kristo” (Warumi 5:17).

Dhambi inapoingia mahali inaleta mauti, magonjwa, uasi, ubishi, umaskini na kutokufanikiwa. Uzima wa milele unapoingia ndani ya mtu unaleta, – Uzima, uponyaji, amani, upendo, utajiri na kufanikiwa na baraka zingine za Mungu. 

UZIMA WA MILELE NA UPONYAJI

Kabla sijampokea Yesu Kristo moyoni mwangu awe Bwana na Mwokozi wangu, nilisumbuliwa sana na magonjwa.

Nakumbuka nilikuwa nasumbuliwa na maumivu ya kichwa mara kwa mara. Nilipokwenda kupimwa hospitali kwa daktari, niliambiwa nina ugonjwa wa vidonda vya tumbo ‘Ulcers’ na pia ‘High blood pressure’. Nilipewa dawa za kutumia, na pia niliambiwa nisile vyakula vya aina fulani maana vitaniongezea ugonjwa.

Niliyafuata masharti ya daktari, na nilipata nafuu kidogo. Lakini kitu cha kushangaza ni kwamba mara kwa mara magonjwa yalinirudia na kunisumbua sana – sikujua kitu cha kufanya. Baada ya miaka kadha neema ya Bwana ilifuniliwa moyoni mwangu, nikaokoka baada ya kutubu na kumpokea Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wangu. Mabadiliko yaliyotokea katika maisha yangu ni makubwa mno. Wakati huo nilikuwa sijajua ni kitu gani kimetokea – lakini nilijua kuwa ninaishi maisha mapya.

Nilishangaa kuona kuwa miezi kadhaa imepita bila kusumbuliwa na magonjwa. Kichwa hakikiniuma tena, moyo uliacha kwenda mbio tena vyakula vingine nilivyokatazwa nisile na daktari havikunidhuru nilipovila tena kama mwanzo. Nilijua hakika kuwa nimepona!

Wakati huo sikuweza kufahamu kitu kilichotokea hata nikapona mara moja namna hiyo. Lakini kwa kadri ambavyo Roho Mtakatifu alivyoendelea kunikuza katika wokovu nilikuja kufahamu ya kuwa MSAMAHA WA DHAMBI UNAONGOZANA NA UPONYAJI WA MWILI.

Kabla ya mwanadamu kutenda dhambi, hakukuwa na magonjwa. Dhambi ilipoingia ilileta na magonjwa pia. Sadaka ya uhai wa Yesu Kristo msalabani ilileta msamaha na ondoleo la dhambi na madhara yake yote ikiwa ni pamoja na MAGONJWA.

Unapompokea Yesu Kristo moyoni mwako kuwa Bwana na Mwokozi wako, unampokea MPONYAJI. Roho wa Uzima wa milele anayeingia kutawala maisha yako, ni Roho wa Uponyaji anayefukuza magonjwa yote ndani yako na kukupa afya.

Ndiyo maana imeandikwa hivi; “Hata kulipokuwa jioni, wakamletea (Yesu Kristo) wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, na KUYACHUKUA MAGONJWA YETU” (Mathayo 8:16,17). Soma pia (Isaya 53:4,5)

Kwa kuwa alichukua dhambi zetu, dhambi hizo zimeondolewa kwetu, na tumepokea utakatifu wake. Kwa kuwa alichukua magonjwa yetu, hakuna sababu ya sisi kuendelea kuumwa kwa kuwa tumepokea uponyaji wake. Ndiyo maana imeandikwa hivi;

“Yeye mwenyewe (Yesu Kristo) alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na KWA KUPIGWA KWAKE MLIPONYWA” (1Petro 2:24).

Angalieni anasema, “ Kwa kupigwa kwake MLIPONYWA” na siyo ‘MTAPONYWA’. Ikiwa TULIPONYWA kwa hiyo sasa TUMEPONA!

Ndiyo maana watu wengi sana nimewasikia wakishuhudia ya kuwa magonjwa yaliyokuwa yanawasumbua kwa muda mrefu yamepona baada ya kumpokea Yesu Kristo mioyoni mwao na kuokoka.

Kuna mama mmoja alinishuhudia ya kuwa alisumbuliwa sana na majini kwa muda wa miaka kumi na mitatu. Alikwenda hospitali – hakupona. Alikwenda kwa waganga wa kienyeji – hakupona. Mwili wake ulidhoofu sana.

Siku moja neema ya Mungu ilimzukia aliamua kuokoka. Mhubiri aliposema watu wanaotaka kuokoka waje mbele, huyo mama naye alikwenda – akafanya sala ya toba na kumkaribisha Yesu Kristo moyoni mwake.

Mama huyo alinambia tangu wakati huo maumivu aliyokuwa nayo mwilini kwa miaka 13 yaliondoka. Mume wake na ndugu zake walishangaa sana. Tangu wakati huo aliookoka na kupona hadi alipokuwa ananisimulia ilikuwa imepita miaka minne, na bado alikuwa amepona na afya njema.

Kama wewe unayesoma haya unaumwa na hujaokoka, nakushauri utubu dhambi zako na umpokee Yesu Kristo moyoni mwako, na DAMU YAKE itakutakasa, na utapokea uponyaji unaouhitaji sasa. Kwa sababu imeandikwa, “ Akusamehe maovu yako yote, akuponya magonjwa yako yote” (Zaburi 103:3). 

UZIMA WA MILELE NA MABADILIKO YA TABIA

Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! Yamekuwa mapya” (2Wakorintho 5:17)

Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi yaani, msamaha wa dhambi”.(Wakolosai 1:13,14).

Yesu Kristo alisema ukiula mwili wake na ukiinywa damu yake yeye anakaa ndani yako na wewe unakaa ndani yake – unapokea uzima wake au uzima wa milele.

Mtu akiwa ndani ya Kristo, anakuwa mtu mpya. Mtu anapokuwa ndani ya Kristo anabadilika tabia yake kwa kuwa amehamishwa toka katika nguvu za giza na tabia yake na kuingia katika ufalme wa Kristo na tabia ya Kikristo.

Mtu akiwa ndani ya Kristo anavua utu wake wa kale na kuvaa utu mpya – anavaa tabia mpya. Wakati fulani nilikuwa mji fulani hapa nchini nikihubiri mkutano wa siku nane, asubuhi moja alikuja mzee mmoja kuniona katika hotel niliyokuwa ninakaa.

Yule mzee akasema; “ Unakumbuka jana ulipoita watu wanaotaka kuokoka waje mbele waombewe, kuna mtoto mmoja alikuwa wa kwanza kufika mbele”.

Ndiyo, nakumbuka”; Nikamjibu.

Yule mzee akaendelea kusema; “Yule mtoto ni wa kwangu, na tangu jana kumetokea mabadiliko makubwa mno ya tabia, nikaona heri nije nikushirikishe”.

Nikamuuliza, “Kumetokea mabadiliko gani?

Huyu mtoto wangu”; yule mzee alieleza; “Kabla ya jana alipoamua kuokoka, alikuwa si mtii, alikuwa hapendi usafi, alikuwa hawezi hata kutandika kitanda chake akiamka asubuhi. Hata tukimwambia afagie uwanja unaozunguka nyumba yetu alikuwa hasikii. Kweli, tumempiga fimbo mpaka tuliogopa tutamuumiza. Lakini kuanzia jana alipookoka (sisi tulifikiri anatania) tabia yake imebadilika kabisa. Amekuwa mtii, kazi anajituma kufanya, amekuwa msafi, hata wakati wa usiku, anachukua biblia na kusali yeye mwenyewe – maajabu haya”.

Usikose Muendelezo wa Somo hili Jumatano ya Wiki Ijayo.