Advertise Here

Friday, April 12, 2013

Papa Francis kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu, Kanisa la Mt. Paulo Jumapili hii.

Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili, tarehe 14 Aprili 2013 kuanzia saa 11:30 jioni, anatarajiwa kutembelea Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, nje ya Kuta za Roma na baadaye, kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu. Katika Maadhimisho ya Ibada hii, Baba Mtakatifu atasaidiana na Kardinali James Michael Harvey, Kardinali Codero Lanza di Montezemolo, Kardinali Francesco Monterisi pamoja na Abate Edmund Power, OSB.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili iliyopita majira ya jioni aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma na kuanza utume wake rasmi kama Askofu wa Jimbo la Roma. Ibada hii ilihudhuriwa na umati mkubwa wa watu waliokuwa wamefurika ndani na nje.

Kama inavyoonekana kuwa ni sehemu ya utaratibu wake, Baba Mtakatifu Francisko huanza kwa kusalimiana na waamini na watu wenye mapenzi mema, ambao wamekuwa wakifurika katika matukio kama hawa tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa. Huu ni upepo mpya wa imani na matumaini ndani ya Kanisa.