Advertise Here

Monday, September 2, 2013

Safu ya James Kalekwa: Mambo yakupasayo Kujua Juu ya Maamuzi - Part I.

Mwl. James Kalekwa

Utangulizi wa Somo:

Kwasababu ya mazoea ya kufanya maamuzi mara kwa mara, watu wengi wamejikuta wamenaswa kwenye mtego wa kutofahamu upana, kina na ukubwa wa jambo hili muhimu. Kila mwanadamu hufaya maamuzi ya kudumu au ya kitambo (muda mfupi); maamuzi ya mara moja (sudden) au yale yachukuayo muda mrefu kuyafikia. Kwa ujumla wake, maisha ya mwanadamu hutawaliwa na maamuzi. Mfano kutembelea blog hii ni uamuzi, kusoma fundisho hili kwenye blog ni uamuzi, kuamka toka kitandani ni uamuzi, ndoa ni uamuzi, kuokoa ni uamuzi… Ungeweza kuwa tofauti na hivyo ulivyo, lakini sivyo kwasababu ya maamuzi.
Ni jambo la msingi sana kufahamu pia ya kwamba maamuzi huathiri si tu maisha ya mtu husika bali huyagusa mpaka maisha ya wale wanaomuhusu sawasawa na nafasi yake – familia, jamaa, jamii, taifa, taasisi n.k
Kwakuwa maamuzi ni jambo la Muhimu kiasi hiki, fuatana nami kwenye mfululizo wa mafundisho haya juu ya maamuzi ili uwe na ufahamu juu ya nini unakiendea kila fursa ya kufanya maamuzi inapojihudhurisha mbele yako. Watu wasio na maarifa na ufahamu hukutwa na kushangazwa na mambo (they are caught by surprise) pindi yanapoanza kutokea. Ni maombi yangu kwa Mungu kwamba Roho Mtakatifu akusaidie kuyatambua yote haya, kwa jina la Yesu Kristo!

Dhana ya Maamuzi kwenye Neno la Mungu

Yoeli 3:14
“Makutano makubwa, makutano makubwa, wamo katika bonde la kukata maneno! Kwa maana siku ya BWANA i karibu, katika bonde la kukata maneno.”

1 Korintho 6: 5
“Nasema hayo nipate kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima, awezaye kukata maneno ya ndugu zake?”

Matendo ya Mitume 24:22
Basi Feliki aliwaahirisha, kwasababu alijua habari za Njia ile kwa usahihi zaidi, akasema, Lisia jemedari atakapotelemka nitakata maneno yenu.

Mith. 16:10
Kukata maneno huwa katika midomo ya mfalme; Kinywa chake hakitakosa katika hukumu.”

Nabii Yoeli anatutambulisha dhana muhimu sana kwenye maisha ambayo amechagua kuiita “kukata maneno”. Nimeambatanisha mistari mingine ili kupana wigo wa uelewa juu ya dhana ya kukata maneno. Ukiisoma mistari inayotangulia na inayofuata baada ya hiyo niliyoambatanisha hapo, utang’amua mara moja ya kwamba kukata maneno si dhana mpya bali ni neno linalowasilisha maana ya kufikia maamuzi ya kimahakama (kunapokuwa na pande mbili zinazokinzana na inatakiwa pande hizo zifike uelewa wa pamoja “consensus”  juu ya jambo fulani); kufikia neno la mwisho juu ya, ama kuhitimisha  mjadala unaoendelea juu ya hoja fulani… Kwa lugha rahisi na ya kueleweka kwa wengi, maelezo yote hayo yaliyotangulia juu ya dhana ya kukata maneno yanaweza kufupishwa kwa neno hili: kufanya maamuzi
Pia ukitazama kwa umakini utagundua ya kwamba Yoeli anatambulisha mahali “venue” pa kufanyia maamuzi. Si kila mahala ni maalum kwa maamuzi… La hasha! Kuna sehemu maalum kwa shughuli hii, na hiyo sehemu inaitwa “Bonde la Kukata maneno”.  Ili tuweze kumuelewa vyema Yoeli, basi karibu ujifunze juu ya dhana ya mihula mitatu kwenye maisha ya mwanadamu ambayo hiyo itatupa kujua wajibu wetu katika zoezi hili Muhimu… Kufanya maamuzi!

Somo litaendelea Jumatatu Ijayo.....

Somo limeandaliwa na:
Mwl. James Kalekwa
0714 762669/0754917764 
Email: jameskalekwa@gmail.com