Advertise Here

Wednesday, March 27, 2013

Solomon Mukubwa na Faraja Ntaboba wawasili Tanzania kwa Tamasha la Pasaka.

Mwimbaji Faraja Ntaboba kutoka DRC akizungumza kitu mbele ya Waandishi wa Habari Jana
WAKATI muimbaji Sipho Makhabane wa Afrika Kusini akitarajiwa kutua nchini siku ya Ijumaa wiki hii, waimbaji wa nyimbo za injili kutoka Kenya na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), wamewasili jana jijini Dar es Salaa, tayari kwa ajili ya kushiriki katika Tamasha la Pasaka, litakaloanza Machi 31 kwenye Uwanja wa Taifa jijini.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa Kamati Maalumu inayoratibu tamasha hilo la kimataifa, Alex Msama aliwataja waimbaji waliowasili jana kuwa ni Solomoni Mukubwa (Kenya) na Faraja Ntaboba (DRC).
Msama aliwataka wapenzi, mashabiki na wadau wa muziki wa injili kujitokeza kwa wingi katika tamasha hilo, ambalo mgeni rasmi atakuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ili kuunga mkono juhudi za kampuni yake kuandaa tamasha hilo kwa malengo mbalimbali ikiwemo kueneza injili ya Mungu na kusaidia makundi maalumu.
Mwimbaji Solomon Mukubwa kutoka Kenya
Kuhusu waimbaji, Msama alisema kuwa hadi kufikia Ijumaa, wakali wote wa nyimbo za injili kutoka nje watakuwa wamewasili jijini tayari kwa tukio hilo linalosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa Dar es Salaam na mikoa yote ambayo tamasha huilo litarindima.
 
Aidha, mkali wa aina hiyo ya muziki kutoka Kenya, Mukubwa, alisema kuwa amejiandaa vya kutosha katika tamasha la mwaka huu ambalo limebeba ujumbe wa Upendo na Amani.


“Wakati wa Uchaguzi wa Nchini Kenya tuliimba na kuhamasisha Amani na Upendo na kwa kupitia tamasha hili tutaimba nyimbo za kuhamasisha Amani na Upendo hapa Tanzania,” alisema Mukubwa.

Muandaaji wa Tamasha hilo, Bw. Alex Msama
Naye mwimbaji kutoka DRC, Ntaboba alisema kuwa, watu wajitokeze kwa wingi katika tamasha hilo na kupata burudani itakayokwenda sambamba na mafundisho ya dini.

Msama aliongeza kuwa idadi ya waimbaji imeongezeka baada ya kujitokeza kwa nyota mwingine aliyemtaja kwa jina moja la Ntutuma kutoka Kenya, ambapo baada ya tamasha hilo kutikisa kwenye jijini Dar es Salaam, itakuwa zamu ya Dodoma, Iringa, Mbeya, Mwanza kabla ya mashambulizi kuhimishiwa mkoani Mara.