Advertise Here

Friday, March 29, 2013

Thamani ya Kifo cha Yesu pale Msalabani.

 
Shaloom Mpendwa!

Ni jambo la pekee tena kwa Mungu kutufikisha katika maadhimisho ya kumbukumbu za kifo chake na kufufuka kwake yaani pasaka. Kwa kifupi nimeona niandike ujumbe huu ili kukumbushana mambo muhimu kwa habari ya Pasaka.
   
Ni muhimu sana kukumbuka kwamba Yesu alikufa pale msalabani kwa sababu kubwa mbili moja ni ili kurejesha mahusiano ya Mungu na mtu kwa lengo la kumsaidia mtu aishi hapa duniani kwa kusudi la Mungu na pili ili tupate wokovu na kisha kuurithi uzima wa milele.

Biblia katika kitabu cha Mathayo 26:53-54 inasema ‘Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri?’ Kutokana na andiko hili ni vema tukajifunza kwamba;
  • Upendo wake (Yesu) ndio uliomsukuma kuyatoa maisha yake kwa ajili yetu.
  • Yesu alikuwa na uwezo wa kuangamiza askari waliokuja kumkamata, lakini hakufanya hivyo ili andiko/kusudi la Mungu lipate kutimizwa.
  • Ndani ya ufahamu wa Bwana Yesu kulikuwa na mwanadamu, ndio maana kwa kuangalia ‘future’ ya mwanadamu na kusudi la uumbaji wa Mungu ilimlazimu kupitia njia ngumu ya msalaba ili atupate mimi na wewe.
Naam ndugu zangu tujiulize, ni upendo wa namna gani wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Biblia inasema katika kitabu cha Waebrania 2:1-3 Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa. Kwa maana ikiwa lile lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wakovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia’

Katika kuendelea kuonyesha thamani ya kifo cha Yesu pale msalabani Yohana naye aliandika akasema ‘Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata  akamtoa Mwanawe pekee, ila kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye’ Yohana 3:16-17.

Jambo la muhimu ni kwamba Bwana Yesu alikufa na kufufuka ili awalete wengi kwenye ufalme wake. Hivyo basi mpenzi msomaji nakusihi usiichezee neema hii, nakusihi usomapo ujumbe huu wewe ambaye hujaokoka, fanya maamuzi ya kuokoka na wewe unayemjua Mungu maanisha katika wokovu wako.

Twaliabudu na kulisifu jina lako wewe uliyeutoa uhai wako kwa ajili yetu ee Bwana. Ahsante kwa siku njema ya leo ambayo Bwana umeifanya kwa ajili yetu ee Mungu.

Basi ndugu zangu tunapoadhimisha sherehe hizi za pasaka tusiifanye kazi ya Yesu pale msalabani kuwa ni bure, bali kuanzia sasa tusienende kama wamataifa waendavyo bali kama wana wa nuru.

Familia yangu pamoja nami tunawatakia heri ya pasaka, ‘Bwana Mungu awabarikie na kuwalinda’.

Mwl. Patrick Samson Sanga
+255 755 816 800