Advertise Here

Monday, November 4, 2013

Safu ya James Kalekwa: Umejenga Juu ya Mwamba au Mchanga? - Part V


James Kalekwa
Shukrani
Bwana Yesu asifiwe! Naomba nianze mafundisho kwenye safu hii kwanza kwa kumshukuru Mungu kwa kunipatia mke mwema kwaajili ya kulitumikia kusudi lake. Kwangu imekuwa ni furaha na shangwe kubwa sana… Nimekuwa nikisubiri kwa shauku kubwa sana.

Pili niushukuru uongozi na watendaji wa Gospel News Media kwa maombi na maneno ya kunitia moyo kwenye shughuli hii iliyoyabadili maisha yangu. Na zaidi ya hapo ninawiwa kuwashukuru wasomaji wa safu hii wale walioniandikia ujumbe mfupi wa maneno (SMS), email, kunipigia simu na namna zote za mawasiliano. Wamo ambao waliniombea na kunitamkia mema bila kuwasiliana nami moja kwa moja- Nyote mmefanyika baraka kwenye maisha yangu na hasa siku hiyo kubwa kwangu.
        
Mimi na mke wangu tunafurahi sana kumtumikia Mungu pamoja na kila mmoja wenu! Sasa karibu tuambatane kwenye mafundisho haya… Tunakupenda na Mungu anakupenda zaidi.
 
Maneno
Baada ya kujifunza kwa kiasi juu ya mawazo ndani ya Mwamba wa kwanza unaozungumza juu ya milango ya fahamu na kazi zake. Tafadhali niruhusu nikuchukue hatua moja mbele. Baada ya muda kiasi, mawazo yanapofanya kazi ndani ya mtu au mtu anapoyatunza mawazo hayo na kuanza kuyakubali (kwa kujua ama kwa kutokujua), hatua mpya huzaliwa nayo huwa ni hatua ya maneno. Kwahiyo maneno ni mawazo yaliyotamkwa!

Mithali 6:2
"Basi umetegwa kwa maneno ya kinywa chako, umekamatwa kwa maneno ya kinywa chako."

Mithali 12:13
"Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake; Na atarudishiwa matendo ya mikono yake."

Kitu ninachotamani ujifunze hapa ni kwamba “Ukiri wako ndiyo umiliki wako, ukiri wako ndiyo ukomo wako.” – Your confesion is your possesion, your confesion is yout limitation! Kwahiyo kile unachokikiri ndiyo huamua ni kwa kiasi gani uende. 

Kimantiki ni sawa kabisa kwasababu kila unapotamka maneno unajua nani huwa wa kwanza kuyasikia maneno/matamshi hayo? Jibu ni rahisi sana…. Wewe mwenyewe! Kila unapofungua Kinywa kutamka neno, wewe huwa wa kwanza kusikia kile ulichotamka kuliko mtu mwingine yeyote na huenda wewe ukawa muathirika au mfaidikaji wa kwanza juu ya maneno hayo kabla ya mtu yeyote.

Hebu nikuonyeshe mifano kadhaa kabla hatujavuka hatua nyingine: Unafahamu kwenye maisha ya elimu hasa kwenye ngazi za sekondari, kuna wanafunzi ambao walijiona ni wadhaifu kwenye masomo fulani mathalani hesabu/hisabati na kwa kujiona hivyo nimeshuhudia wengi wakijisemea “Mimi nasoma ili nipate D tu ya somo hili.” Au “Mimi si mjuzi sana wa hesabu hivyo ninasoma ili nisipate F”.

Umeshawahi kusikia wanafunzi ambao wamekuwa na maandalizi dhaifu au kwa sababu nyingine yoyote hujisemea “Mimi hata nikipata Division III (Daraja la tatu la ufaulu) inatosha kabisa…”….Je, ndugu hao hupata tofauti sana na ukiri wao? Je, watu wanaweka juhudi zao kusoma ili wapate alama D hujikuta wamepata alama A? Je, ndugu watafutao Division III hujikuta wamepata Division I?

HAPANA!!! Kanuni za kiroho zinaniambia “umetegwa kwa maneno ya kinywa chako”. Ukitamka ya kwamba wewe si mshindi, tafadhali kumbuka kuwa mtu wa kwanza anayesikia na kuelewa vyema sana maana ya taarifa hiyo ni wewe mwenyewe.

Naomba kuweka mkazo sana juu ya jambo muhimu sana: kuwa na ukiri/maneno/matamshi yale yale pasipo kujali mazingira, nyakati, watu – consistence in confesions. Ili uyaone matunda halisi ya kinywa chako unapaswa kutunza ukiri au maneno ya kinywa chako… Unatakiwa kuwa ni mtu mwenye msimamo ule ule wa kimaneno juu ya hali fulani japo utumizi wa lugha unaweza kubadilika lakini maana ya maneno iwe ni ilele.

Kuna kitu kwenye lugha ya kiingereza wanaita “doublé standards” yaani kigeugeu au hali ya kubadilikabadilika kama kinyonga hivi. Kuna ndugu ambao wao hukiri au huwa na maneno yaliyo na utofauti mkubwa sana kama mbingu na nchi juu ya hali zile zile… Yaani maneno yao hukinzana sana juu ya jambo moja ambalo walipaswa kuwa na usemi uleule.

Kwa mfano, kuna ndugu ambao juu ya hali ya uchumi na maendeleo ya maisha yao hukiri kwamba wamefanikiwa na Baadaye hujikuta wanakiri juu ya kutokufanikiwa- huukiri utajiri na Baadaye huukiri umaskini.

Yaani mtu wa namna hii akikaa na ndugu wanaowaza na kukiri utajiri hujikuta anakiri vivyo hivyo au anafanania na wanaokiri utajiri na kisha mtu huyo huyo akijikuta mingoni mwa ndugu wanaopenda kuukiri umaskini juu ya maisha yao naye hujikuta anakiri umaskini!

Kwahiyo ni dhahri ya kwamba mtu huyo hana ukiri mmoja (consistence in confesion) juu ya hali ya kiuchumi… Ni mtu mwenye kigeugeu! Mungu akusaidie sana usiwe na namna hiyo ya maisha! Tunza sana ukiri wako, tunza sana maneno ya kinywa chako.


1 Timotheo 6: 13

“Nakuagiza mbele za Mungu anayevihifadhi hai vitu vyote, na mbele za Kristo Yesu, aliyeyaungama maungamo mazuri yale mbele ya Pontio Pilato.”

Biblia ya kiswahili inatumia neno “maungamo” ambalo miongoni mwa watu wengi hujenga dhana ya toba au kujutia dhambi na kuomba msamaha! Lakini kwenye mstari huu haimaanishi hivyo… Si unajua Yesu hakutenda dhambi na hakuwahi kuwa mwenye dhambi? Kwahiyo mbele ya Pilato hakuwa anatoa maungamo uyajuayo…

Kwa kutumia mwanga/ufahamu wa vitabu vya Injili (Yohana sura ya 18&19; Luka sura ya 23; Marko sura ya 15 na Mathayo sura ya 27). Nakushauri ukipata muda usome kwenye injili hizo. Yesu hakukinzana katika ukiri wake- ndiyo yake ilikuwa ni ndiyo na hapana yake ilikuwa ni hapana.

Haijalishi nani alisimama mbele yake, haijalishi nani alimuhoji maswali, haijalishi vitisho au mazingira aliyokuwamo hakubadili ukiri wake… Aliungama maungamo yaliyo mema! Na matokeo yake, Yesu ni sawa sawa na maungamo yake… Alikiri juu ya ufalme, aliungama juu ya mamlaka aliyonayo, alitamka juu uungu wake na “akashiba matunda ya kinywa chake”! Hatimaye akawa sawasawa na ukiri wake – He eventually became as His confesión!

Kitu ninachotamani sana ndani ya moyo wangu kiumbike na kufanyika halisi kwako ni kwamba asikudanganye mtu – huwezi kuwa tofauti na ukiri wako! Kuna watu wanomba na kumwamini Mungu juu ya kupata wenzi wa kuwafaa kwenye maisha yao kisha baada ya Maombi wanaungana  na wanadamu wa kawaida kulalamika na kukiri “Siku hizi hakuna mapenzi, hakuna upendo… sidhani kama nitapata mwenzi.”.

Kwa ukiri huo wanayafuta Maombi waliyowekeza muda wao mwingi! Ndugu, usiwe kigeugeu, usiwe na “double standards” ndiyo yako na iwe ndiyo, na siyo yako na iwe siyo!
Kumbuka sana maneno hukuwekea wewe ukomo/mipaka ya utendaji wako…

Huwezi kuyavuka! Kwahiyo ningependa kukushauri ya kwamba ni heri ukatumia muda wako kujibidiisha kulijua neno la Mungu na baada ya hapo uanze kulikiri neno la Mungu juu ya hali mbali mbali za maisha na hilo ndilo lifanyike ukiri wako. 

Somo litaendelea Jumatatu Ijayo.....

 Mafundisho haya yameandaliwa na James Kalekwa
Mwanataaluma, Mwandishi wa vitabu na Mwalimu wa Neno la Mungu
+255 714 762 669
+255 754 917 764