Advertise Here

Saturday, November 16, 2013

Kasisi atekwa huko Cameroon.

Kasisi mmoja mfaransa ametekwa nyara Kaskazini mwa Cameroon karibu na mpaka wa Nigeria. Taarifa hii ni kwa mujibu wa Wizara ya mambo ya nje ya Ufaransa.

Kasisi huyo, Georges Vandenbeusch alitekwa nyara mapema asubuhi mnamo siku ya Alhamisi, umbali wa kilomita 30 kutoka mpakani.

Takriban watu 15 waliokuwa wamejihami, walivamia makao ya Nguetchewe ambako kasisi huyo alikuwa akifanya kazi , kulingana na Askofu mkuu.

Kundi la wapiganaji wa Boko Haram, wanajulikana kuendeshea harakati zao katika eneo hilo.

Askofu mkuu ambaye kasisi huyo alikuwa chini yake, alisema kua kijisanduku cha kasisi huyo kilipatikana barabarani.

Baadhi ya waliofanya kazi na kasisi huyo walisema kuwa watekaji nyara walifika kwa miguu kumteka nyara kasisi na kuwa walikuwa wanaongea kiingereza.

Msemaji wa serikali ya Cameroon, Issa Tchiroma Bakary, alisema kuwa maafisa wanahofia kwamba kasisi huyo tayari ameondolewa nchini.

Kwa mujibu wa maafisa wakuu, huenda wapiganaji wa Boko Haram ndio waliomteka kasisi huyo.

Rais Francois Hollande, amesema kuwa wanafanya kila hali kuhakikisha kuwa kasisi huyo ataachiliwa.

Akizungumza mjini Monaco, aliwasihi raia wa Ufansa kutohatarisha maisha yao.

Mapema mwaka huu, jamaa saba wa familia moja , wanne kati yao watoto, walitekwa nyara na wapiganaji wa kiisilamu na kuzuiliwa kwa miezi miwili.

- BBC Swahili -